Habakuki 2

Habakuki 2

1Mimi nitasimama mahali pa kuchungulia,

na kukaa juu mnarani;

nitakaa macho nione ataniambia nini,

atajibu nini kuhusu lalamiko langu.”

Mungu anamjibu Habakuki

2Kisha, Mwenyezi-Mungu akanijibu hivi:

“Yaandike maono haya;

yaandike wazi juu ya vibao,

anayepitia hapo apate kuyasoma.

3Maono haya yanangoja wakati wa kufaa;[#Taz Ebr 10:37]

ni maono ya ukweli juu ya mwisho.

Kama yaonekana kuchelewa, uyasubiri;

hakika yatafika, wala hayatachelewa.

4Andika:[#Taz Roma 1:17; Gal 3:11; Ebr 10:38]

‘Waangalie wenye kiburi, hao wataangamia;

lakini waadilifu wataishi kwa kumwamini Mungu.’”

Waovu wataangamia

5Zaidi ya hayo, divai hupotosha;

mtu mwenye kiburi hatadumu.

Yuko tayari kuwameza wengine kama Kuzimu;

kama vile kifo, hatosheki na kitu.

Hujikusanyia mataifa yote,

na watu wote kama mali yake.

6Kila mtu atamdhihaki mtu wa namna hiyo

na kumtungia misemo ya dhihaka:

“Ole wako unayejirundikia visivyo vyako,

na kuchukua rehani mali za watu lakini hulipi!

Utaendelea kufanya hivyo hadi lini?

7Siku moja wadeni wako watainuka ghafla,

wale wanaokutetemesha wataamka.

Ndipo utakuwa mateka wao.

8Wewe umeyapora mataifa mengi,

lakini wote wanaosalimika watakupora wewe,

kwa mauaji na dhuluma uliyoitendea dunia,

naam, uliyoifanyia miji na wakazi wake wote.

9“Ole wako unayejitajirisha kwa hasara ya mwingine,

ujengaye nyumba yako juu milimani

ukidhani kuwa salama mbali na madhara.

10Lakini kwa mipango yako umeiaibisha jamaa yako.

Kwa kuyaangamiza mataifa mengi,

umeyaangamiza maisha yako mwenyewe.

11Ndiyo maana hata mawe yatalalamika ukutani,

na boriti za nyumba zitayaunga mkono.

12“Ole wako unayejenga mji kwa mauaji

unayesimika jiji kwa maovu!

13Mwenyezi-Mungu wa majeshi husababisha

juhudi za watu zipotelee motoni,

na mataifa yajishughulishe bure.

14Utukufu wa Mwenyezi-Mungu utaenea pote duniani,[#Taz Isa 11:9]

kama vile maji yaeneavyo baharini.

15Ole wako unayewalewesha jirani zako,

na kutia sumu katika divai yao

ili upate kuwaona wamekaa uchi.

16Utajaa aibu badala ya heshima.

Utakunywa wewe mwenyewe na kupepesuka!

Mwenyezi-Mungu mwenyewe atakulevya,

na aibu itaifunika heshima yako!

17Maovu uliyoitenda Lebanoni yatakuvamia wewe;

uliwaua wanyama, wanyama nao watakutisha.

Yote hayo yatakupata wewe,

kwa mauaji na dhuluma uliyoitendea dunia,

naam, uliyoifanyia miji na wakazi wake wote.

18“Chafaa nini kinyago alichotengeneza mtu?

Sanamu ni madini yaliyoyeyushwa,

ni kitu cha kueneza udanganyifu!

Mtengeneza sanamu hutumaini alichotengeneza mwenyewe,

kinyago ambacho hakiwezi hata kusema!

19Ole wake mtu aliambiaye gogo: ‘Amka!’

Au jiwe bubu ‘Inuka!’

Je, sanamu yaweza kumfundisha mtu?

Tazama imepakwa dhahabu na fedha,

lakini haina uhai wowote.”

20Lakini Mwenyezi-Mungu yumo katika hekalu lake takatifu;

dunia yote na ikae kimya mbele yake.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania