Yohane 12

Yohane 12

Yesu anapakwa marashi

(Mat 26:6-13; Marko 14:3-9)

1Siku sita kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu alifika Bethania alikoishi Lazaro ambaye Yesu alikuwa amemfufua kutoka wafu.

2Huko walimwandalia chakula cha jioni, naye Martha akawa anawatumikia. Lazaro alikuwa mmoja wa wale waliokuwa mezani pamoja na Yesu.

3Basi, Maria alichukua nusu lita ya marashi ya nardo safi ya thamani kubwa, akampaka Yesu miguu na kuipangusa kwa nywele zake. Nyumba yote ikajaa harufu ya marashi.[#12:3 Nardo ni mmea ulioota kaskazini ya India; mizizi ya mmea huo ilitumiwa kutengenezea mafuta ya marashi ya harufu nzuri sana.]

4Basi, Yuda Iskarioti, mmoja wa wale kumi na wawili ambaye ndiye atakayemsaliti Yesu, akasema,[#12:4 Huyu alikuwa mwanafunzi ambaye alitunza mfuko wa fedha zilizotumika kwa mahitaji ya Yesu na wanafunzi wake na pia kusaidia maskini.]

5“Kwa nini marashi hayo hayakuuzwa kwa fedha dinari 300, wakapewa maskini?”[#12:5 Yaani kiasi cha mshahara wa mwaka mzima wa kibarua wakati huo.]

6Alisema hivyo, si kwa kuwa alijali chochote juu ya maskini, bali kwa sababu alikuwa mweka hazina, na kwa kuwa alikuwa mwizi, mara kwa mara aliiba kutoka katika hiyo hazina.

7Lakini Yesu akasema, “Msimsumbue huyu mama! Mwacheni ayaweke kwa ajili ya siku ya mazishi yangu.[#12:7 Yesu anafafanua kitendo cha huyo mama kama kinachoashiria kupakwa kwake mafuta baada ya kifo chake. Anakithamini kitendo hicho na kumtetea huyo mama dhidi ya lawama za Yuda. Katika Mathayo na Marko wanafunzi wote wanamsuta Maria.]

8Maskini mtakuwa nao siku zote, lakini hamtakuwa nami siku zote.”

Njama za kumwua Lazaro

9Wayahudi wengi walisikia kwamba Yesu alikuwa Bethania. Basi, wakafika huko si tu kwa ajili ya kumwona Yesu, ila pia wapate kumwona Lazaro ambaye Yesu alimfufua kutoka kwa wafu.

10Makuhani wakuu waliamua pia kumwua Lazaro,

11maana kwa sababu ya Lazaro Wayahudi wengi waliwaasi viongozi wao, wakamwamini Yesu.

Yesu anaingia Yerusalemu kwa shangwe

(Mat 21:1-11; Marko 11:1-11; Luka 19:28-40)

12Kesho yake, kundi kubwa la watu waliokuja kwenye sikukuu walisikia kuwa Yesu alikuwa njiani kuja Yerusalemu.

13Basi, wakachukua matawi ya mitende, wakatoka kwenda kumlaki; wakapaza sauti wakisema:[#12:13 Matawi ya mitende yalitumika mara kwa mara kuwakaribisha watu maarufu au watawala waliofika Yerusalemu.]

“Sifa! Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Bwana.

Abarikiwe mfalme wa Israeli.”

14Yesu akampata mwanapunda mmoja, akapanda juu yake kama yasemavyo Maandiko:

15“Usiogope mji wa Siyoni!

Tazama, Mfalme wako anakuja,

amepanda mwanapunda!”

16Wakati huo wanafunzi wake hawakuelewa mambo hayo, lakini Yesu alipokwisha tukuzwa, ndipo walipokumbuka kwamba hayo yalikuwa yameandikwa juu yake, na kwamba watu walikuwa wamemtendea hivyo.

17Kundi la watu wale waliokuwa pamoja na Yesu wakati alipomwita Lazaro kutoka kaburini, akamfufua kutoka kwa wafu, walimshuhudia.

18Kwa hiyo umati huo wa watu ulimlaki, maana wote walisikia kwamba Yesu alikuwa amefanya ishara hiyo.

19Basi, Mafarisayo wakaambiana, “Mnaona? Hatuwezi kufanya chochote! Tazameni, ulimwengu wote unamfuata.”

Wagiriki kadhaa wanataka kumwona Yesu

20Kulikuwa na Wagiriki kadhaa miongoni mwa watu waliokuwa wamefika Yerusalemu kuabudu wakati wa sikukuu hiyo.[#12:20 Huenda hawa walikuwa watu wasio Wayahudi ambao waliabudu Mungu pamoja na Wayahudi. Na kuhusu Filipo (ambaye huenda aliongea Kigiriki na hiyo inaweza kueleweka kwa nini walimwendea) taz 1:45 maelezo.]

21Hao walimwendea Filipo, mwenyeji wa Bethsaida katika Galilaya, wakasema, “Mheshimiwa, tunataka kumwona Yesu.”

22Filipo akaenda, akamwambia Andrea, nao wawili wakaenda kumwambia Yesu.

23Yesu akawaambia, “Saa ya kutukuzwa kwa Mwana wa Mtu imefika![#12:23 Taz Yoh 2:4 kuhusu saa yake Yesu na 7:39 kuhusu kutukuzwa kwake.]

24Kweli nawaambieni, punje ya ngano hubaki punje tu isipokuwa ikianguka katika udongo na kufa. Kama ikifa, basi huzaa matunda mengi.

25Anayependa maisha yake, atayapoteza; anayeyachukia maisha yake katika ulimwengu huu, atayaweka kwa ajili ya uhai wa milele.

26Anayetaka kunitumikia ni lazima anifuate, hivyo kwamba popote pale nilipo mimi ndipo na mtumishi wangu atakapokuwa. Mtu yeyote anayenitumikia Baba yangu atampa heshima.

Yesu anasema juu ya kifo chake

27“Sasa roho yangu imefadhaika, na niseme nini? Je, niseme: ‘Baba, usiruhusu saa hii inifikie?’ Lakini ndiyo maana nimekuja — ili nipite katika saa hii.[#12:27-28 Hii sala ya Yesu inafanana na ile inayotajwa katika zile Injili nyingine tatu bustanini Gethsemane (Mat 26:39; Marko 14:36; Luka 22:42). Yesu anajua kwamba atatimiza matakwa ya Mungu kwa mateso na kifo msalabani.]

28Baba, ulitukuze jina lako.” Hapo sauti ikasema kutoka mbinguni, “Nimelitukuza, na nitalitukuza tena.”[#12:28 Sauti hiyo ilitoka kwa Mungu, lakini wengine walisema ilikuwa ngurumo au sauti ya malaika (aya 29). Katika Biblia mara nyingine ngurumo huambatishwa na sauti ya Mungu (Kut 19:6; Zab 29; 1Sam 7:9-10; Ufu 14:2).]

29Umati wa watu waliokuwa wamesimama hapo walisikia sauti hiyo, na baadhi yao walisema, “Ni ngurumo.” Lakini wengine wakasema, “Malaika ameongea naye!”

30Lakini Yesu akawaambia, “Sauti hiyo haikutokea kwa ajili yangu mimi, ila kwa ajili yenu.

31Sasa ndio wakati wa ulimwengu huu kuhukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atapinduliwa.[#12:31 Hii ni namna ya mwandishi ya kumtaja Ibilisi au Shetani ambaye kwa kawaida anafahamika kama kiongozi wa nguvu za uovu zinazopingana na Mungu na watu wake. Taz 8:44; 14:30 na 16:11. Katika Injili hii ya Yohane neno “ulimwengu” mara nyingine linahusu watu wanaoishi humu ulimwenguni na pia nguvu za uovu ambazo hujaribu kudhibiti maisha yao.]

32Nami nitakapoinuliwa juu ya nchi nitamvuta kila mmoja kwangu.”[#12:32 Wazo kuu hapa sio tu kuwekwa juu ya msalaba bali pia lile wazo la kuinuliwa kutoka kifo na kufufuliwa. Taz, k.m. 1Tim 3:16 na pia Luka 9:51 na Fil 2:9 ambapo kutukuzwa kwake kwahusika.]

33(Kwa kusema hivyo alionesha atakufa kifo gani).

34Basi, umati huo ukamjibu, “Sisi tunaambiwa na sheria yetu kwamba Kristo atadumu milele. Wawezaje basi, kusema ati Mwana wa Mtu anapaswa kuinuliwa? Huyo Mwana wa Mtu ni nani?”[#12:34 Hakuna mahali kamili katika A.K. ambapo inasemwa Kristo (au Masiha) atadumu milele lakini taz Zab 89:4,36; 110:4; Isa 9:7; Eze 37:25. Inawezekana pia.]

35Yesu akawaambia, “Mwanga bado uko nanyi kwa muda mfupi. Tembeeni mngali mnao huo mwanga ili giza lisiwapate; maana atembeaye gizani hajui aendako.

36Basi, wakati mnao huo mwanga uaminini ili mpate kuwa watu wa mwanga.” Baada ya kusema maneno hayo, Yesu alikwenda zake na kujificha mbali nao.

Watu hawana imani

37Ingawa Yesu alifanya miujiza hii yote mbele yao, wao hawakumwamini.

38Hivyo maneno aliyosema nabii Isaya yakatimia:

“Bwana, nani aliyeuamini ujumbe wetu?

Na uwezo wa Bwana umedhihirishwa kwa nani?”

39Hivyo hawakuweza kuamini, kwani Isaya alisema tena:

40“Mungu ameyapofusha macho yao,

amezipumbaza akili zao;

wasione kwa macho yao,

wasielewe kwa akili zao;

wala wasinigeukie, asema Bwana,

ili nipate kuwaponya.”

41Isaya alisema maneno haya kwa sababu aliuona utukufu wa Yesu, akasema habari zake.

42Hata hivyo, wengi wa viongozi wa Wayahudi walimwamini Yesu. Lakini kwa sababu ya Mafarisayo, hawakumkiri hadharani kwa kuogopa kwamba watatengwa na sunagogi.

43Walipendelea kusifiwa na watu kuliko kusifiwa na Mungu.

Yesu alikuja kuuokoa ulimwengu

44Kisha Yesu akasema kwa sauti kubwa, “Mtu anayeniamini, haniamini mimi tu, ila anamwamini pia yule aliyenituma.

45Anayeniona mimi anamwona pia yule aliyenituma.

46Mimi ni mwanga, nami nimekuja ulimwenguni ili wote wanaoniamini wasibaki gizani.

47Anayeyasikia maneno yangu lakini hayashiki, mimi sitamhukumu; maana sikuja kuuhukumu ulimwengu bali kuuokoa.[#12:47 Taz 3:17; 8:15.]

48Asiyeyashika maneno yangu anaye wa kumhukumu: neno lile nililosema ni hakimu wake siku ya mwisho.

49Mimi sikunena kwa mamlaka yangu mwenyewe, ila Baba aliyenituma ndiye aliyeniamuru niseme nini na niongee nini.

50Nami najua kuwa amri yake huleta uhai wa milele. Basi, mimi nasema tu yale Baba aliyoniagiza niyaseme.”

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania