Zaburi 120

Zaburi 120

Kuomba msaada

1Katika taabu yangu nilimwita Mwenyezi-Mungu,

naye akanijibu.

2Uniokoe ee Mwenyezi-Mungu,

na watu wadanganyifu na waongo.

3Enyi watu wadanganyifu, mtapewa kitu gani?

Mtaadhibiwa namna gani?

4Kwa mishale mikali ya askari,

kwa makaa ya moto mkali!

5Ole wangu kwamba naishi kama mgeni huko Mesheki;[#120:5 “Mesheki” ulidhaniwa kuwa mji au eneo karibu na Bahari ya Kaspia na “Kedari” eneo au mji katika jangwa kusini mwa Damasko katika Siria. Kwa sababu ya umbali kati ya maeneo hayo mawili wafafanuzi wanafikiri majina hayo yanatumiwa kama mfano: watu wa Mesheki na Kedari walidhaniwa kuwa watu wabaya sana, watu wanaochukia amani au wasiopenda kutenda haki.]

naishi kama mgeni katika mahema ya Kedari.

6Nimeishi muda mrefu mno

kati ya watu wanaochukia amani!

7Wakati ninaposema nataka amani,

wao wanataka tu vita.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania