Zaburi 143

Zaburi 143

Sala ya kuomba msaada

1Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu!

Ulitegee sikio ombi langu

maana wewe ni mwaminifu;

unijibu kwa sababu ya uadilifu wako.

2Usinitie hukumuni mimi mtumishi wako,

maana hakuna yeyote aliye mwadilifu mbele yako.

3Maadui zangu wamenifuatia;

wameniangusha chini kabisa

wameniketisha gizani kama mtu aliyekufa zamani.

4Nimevunjika moyo kabisa;

nimekufa ganzi kwa ajili ya woga.

5Nakumbuka siku zilizopita;

natafakari juu ya yote uliyotenda,

nawaza na kuwazua juu ya matendo yako.

6Nakunyoshea mikono yangu kuomba;

nina kiu yako kama nchi kavu isiyo na maji.

7Ee Mwenyezi-Mungu, unijibu haraka;

maana nimekata tamaa kabisa!

Usijifiche mbali nami,

nisije nikawa kama wale washukao kwa wafu.

8Asubuhi unioneshe fadhili zako,[#143:8 Wakati wa matumaini mapya baada ya usiku wa giza la kukata tamaa.]

maana nimekuwekea tumaini langu.

Unifundishe mwenendo wa kufuata,

maana nakuelekezea ombi la moyo wangu.

9Uniokoe, ee Mwenyezi-Mungu, kutoka maadui zangu,

maana kwako nakimbilia usalama.

10Unifundishe kutimiza matakwa yako,

maana wewe ni Mungu wangu!

Roho yako nzuri iniongoze katika njia sawa.

11Unifadhili, ee Mwenyezi-Mungu, kwa hisani yako,

uniondoe katika taabu kwa sababu ya uadilifu wako.

12Kwa sababu ya fadhili zako uwakomeshe maadui zangu,

uwaangamize wote wanaonidhulumu;

maana mimi ni mtumishi wako.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania