Zaburi 84

Zaburi 84

Hamu ya kuwa nyumbani kwa Mungu

1Jinsi gani yanavyopendeza makao yako,[#84:1 Taz pia Zab 42 na 43 kuhusu namna hii ya kusema. Na kuhusu jina la sifa “Mwenyezi-Mungu wa Majeshi” taz Zab 46:7 maelezo.]

ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi!

2Nafsi yangu yatamani mno maskani ya Mwenyezi-Mungu!

Moyo na mwili wangu wote wamshangilia Mungu aliye hai.

3Hata shomoro wamepata makao yao,[#84:3 Mwanazaburi huyu anaona wivu juu ya ndege ambao wanaruka bila kuzuiwa katika hekalu.]

mbayuwayu wamejenga viota vyao,

humo wameweka makinda yao,

katika madhabahu zako, ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi,

Mfalme wangu na Mungu wangu!

4Heri wale wanaokaa nyumbani mwako,[#84:4 Hao au ni maofisa wa hekalu kama vile Walawi au ni njia ya kusema juu ya watu ambao huzoea kuabudu hekaluni.]

wakiimba daima sifa zako.

5Heri watu wanaopata nguvu zao kwako,

wanaotamani kwenda kuhiji mlimani kwako.

6Wapitapo katika bonde kavu la Baka,[#84:6 Mahali penyewe hapajulikani.]

hulifanya kuwa mahali pa chemchemi,

na mvua za vuli hulijaza madimbwi.

7Wanaendelea kupata nguvu zaidi na zaidi;

watamwona Mungu wa miungu huko Siyoni.

8Usikie sala yangu ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi;

unitegee sikio, ee Mungu wa Yakobo.

9Ee Mungu, umwangalie kwa wema ngao yetu mfalme,[#84:9 Jina hili ngao (likiwa na maana ya mlinzi) pamoja na “huyo uliyemweka wakfu” (taz 2:2 maelezo) yote yanamtaja mfalme wa Waisraeli.]

umtazame huyo uliyemweka wakfu kwa mafuta.

10Siku moja tu katika maskani yako,

ni bora kuliko siku elfu mahali pengine;

afadhali kusimama mlangoni pa nyumba yako,

kuliko kuishi nyumbani kwa watu waovu.

11Mwenyezi-Mungu ni jua letu na ngao yetu;

yeye hutuneemesha na kutujalia fahari.

Hawanyimi chochote kilicho chema,

wale waishio kwa unyofu.

12Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi,

heri mtu yule anayekutumainia wewe!

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania