The chat will start when you send the first message.
1Basi Sarai, mkewe Abramu, alikuwa hajamzalia watoto. Lakini alikuwa na mjakazi Mmisri jina lake Hajiri.
2Hivyo Sarai akamwambia Abramu, “Bwana amenizuilia kupata watoto. Basi nenda ukutane kimwili na mjakazi wangu; huenda nitaweza kupata watoto kupitia kwake.”
Abramu akakubaliana na lile Sarai alilosema.
3Hivyo baada ya Abramu kuishi katika nchi ya Kanaani miaka kumi, Sarai akamchukua mjakazi wake Mmisri aliyeitwa Hajiri, na kumpa mumewe awe mke wake.
4Abramu akakutana kimwili na Hajiri, naye akapata mimba.
Hajiri alipojua kuwa ana mimba, akaanza kumdharau Sarai.
5Ndipo Sarai akamwambia Abramu, “Unawajibika na mateso ninayoyapata. Nilimweka mtumishi wangu mkononi mwako. Sasa kwa vile anajua kwamba ana mimba, ananidharau mimi. Bwana na aamue kati yako na mimi!”
6Abramu akamwambia, “Haya, mtumishi wako yuko mkononi mwako. Mtendee lolote utakalo!” Ndipo Sarai akamtesa Hajiri, naye akamtoroka.
7Malaika wa Bwana akamkuta Hajiri karibu na chemchemi huko jangwani; chemchemi hiyo ilikuwa kando ya barabara iendayo Shuri.
8Malaika akamwambia, “Hajiri, mtumishi wa Sarai, umetoka wapi, na unaenda wapi?”
Akamjibu, “Ninamkimbia bibi yangu Sarai.”
9Ndipo malaika wa Bwana akamwambia, “Rudi kwa bibi yako ukajishushe chini yake.”
10Malaika akaendelea akasema, “Nitazidisha wazao wako, hivi kwamba watakuwa wengi mno wasiohesabika.”
11Pia malaika wa Bwana akamwambia:
“Wewe sasa una mimba
nawe utamzaa mwana.
Utamwita jina lake Ishmaeli,
kwa sababu Bwana amesikia kuhusu huzuni yako.
12Atakuwa kama punda-mwitu kati ya wanadamu;
mkono wake utakuwa dhidi ya kila mtu,
na mkono wa kila mtu utakuwa dhidi yake,
naye ataishi kwa uhasama
na ndugu zake wote.”
13Hajiri akampa Bwana aliyezungumza naye jina hili: “Wewe ndiwe Mungu unionaye mimi,” kwa maana alisema, “Sasa nimemwona yeye anayeniona mimi.”
14Ndiyo sababu kisima kile kikaitwa Beer-Lahai-Roi; bado kipo hata leo kati ya Kadeshi na Beredi.[#16:14 maana yake Yeye Aliye Hai Anionaye]
15Hivyo Hajiri akamzalia Abramu mwana, naye Abramu akamwita huyo mwana Hajiri aliyemzalia jina la Ishmaeli.
16Abramu alikuwa na umri wa miaka themanini na sita Hajiri alipomzalia Ishmaeli.