Yoshua Mwana wa Sira 1

Yoshua Mwana wa Sira 1

MKUSANYO WA MITHALI

Kusifu Hekima

1Hekima yote yatoka kwa BWANA,[#Mit 2:6]

Nayo yakaa kwake hata milele.

2Nani awezaye kuhesabu

Mchanga wa bahari na matone ya mvua

Na siku za milele?

3Nani awezaye kutafuta

Kimo cha mbingu na upana wa dunia

Na kina cha bahari?

4Hekima iliumbwa kabla ya vitu vyote,

5Na ufahamu wa busara tangu milele.

6Nani aliyefunuliwa shina la hekima?

7Nani aliyejua mashauri yake merevu?

8Yuko Mmoja aliye na hekima,

Naye yu wa kuogopwa sana,

Ameketi katika kiti chake cha enzi.

9BWANA ndiye aliyeiumba[#Mit 8:22-31; Sira 29:9]

Na kuiona na kuihesabu,

Na kuimwaga juu ya kazi zake zote.

10Ina wote wenye mwili kama aitoavyo,

Na wale wampendao amewapa kwa wingi.

Kumcha Mungu ni Hekima ya Kweli

11Kumcha BWANA

Ni heshima na utukufu,

Na furaha na taji la shangwe.

12Kumcha BWANA

Kunachangamsha moyo,

Na kuleta sherehe na maisha kunjufu.

13Kumcha BWANA

Kwamletea mtu heri mwishowe,

Na siku ya kufa kwake atabarikiwa.

14Kumcha BWANA

Ni chanzo cha hekima,

Imeumbwa tumboni pamoja na waamini.

15Kwa watu imekaa tangu awali,

Pia itadumu kwa wazao wao.

16Kumcha BWANA

Ni utimilifu wa hekima,

Inashibisha wanadamu matunda yake.

17Itajaza nyumba pia vitakiwavyo,[#Hek 7:11]

Na ghala zitajazwa mavuno yake.

18Kumcha BWANA

Ni taji la hekima,

Inasitawisha amani na afya nzuri.

19Kumcha BWANA

Ni gongo na nguzo tukufu,

Ni heshima ya daima kwao waishikao.

20Kumcha BWANA[#Mit 3:16; 4:10]

Ni shina la hekima,

21Na matawi yake ni maisha mengi.

Saburi na kujiweza

22Hasira isiyo haki haiwezi kuthibitishwa,

Maana ukali wa ghadhabu ni maangamizi yake.

23Mtu aliye mvumilivu atastahimili hata wakati ufaao, na hatimaye ukunjufu wa moyo utaanza kukua ndani yake.

24Aidha, ujapo wakati ufaao atayaficha maneno yake, na wengi kwa midomo yao watautangaza ufahamu wake.

Hekima na unyofu

25Mithali za elimu zimo kazini mwa hekima,

Bali utawa ni chukizo kwa mkosefu.

26Ukitamani hekima uzishike amri, naye BWANA atakupa tele;

27yaani, kumcha BWANA ndiyo hekima na mafundisho, tena imani na unyenyekevu ndiyo mapenzi yake.

28Usikatae kumcha BWANA kama una haja,

Wala usimkaribie nawe una nia mbili.

29Usiwe mnafiki machoni pa watu, tena kuhusu midomo yako ufanye hadhari.

30Wewe usijikuze mwenyewe, usije ukaanguka na kujiaibisha roho yako; madhali BWANA atazifunua siri zako, na kukuangamiza katikati ya kusanyiko, kwa sababu hukumfikilia BWANA mwenye kicho, lakini moyo wako umejaa hila.

The Holy Bible in Kiswahili, Revised Union Version © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 2013. 
Published by: Bible Society of Tanzania