Methali 16

Methali 16

1Binadamu hupanga mipango yake,

lakini kauli ya mwisho ni yake Mwenyezi-Mungu.

2Matendo ya mtu huonekana kwake kuwa sawa,

lakini Mwenyezi-Mungu hupima nia ya mtu.

3Mwekee Mwenyezi-Mungu kazi yako,

nayo mipango yako itafanikiwa.

4Mwenyezi-Mungu ameumba kila kitu kwa kusudi lake;

hata waovu kwa ajili ya siku ya maangamizi.

5Kila mwenye kiburi ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu;

hakika mtu wa namna hiyo hataacha kuadhibiwa.

6Kwa utii na uaminifu mtu huondolewa dhambi,

kwa kumcha Mwenyezi-Mungu huepuka uovu.

7Mwenyezi-Mungu akipendezwa na mwenendo wa mtu,

huwageuza hata adui zake kuwa marafiki.

8Afadhali mali kidogo kwa uadilifu,

kuliko mapato mengi kwa udhalimu.

9Mtu aweza kufanya mipango yake,

lakini Mwenyezi-Mungu huongoza hatua zake.

10Mfalme huamua kwa maongozi ya Mungu;

anapotoa hukumu hakosei.

11Mwenyezi-Mungu hutaka kipimo na mizani halali;

mawe yote mfukoni ya kupimia ni kazi yake.

12Ni chukizo kubwa wafalme kutenda uovu,

maana msingi wa mamlaka yao ni haki.

13Mfalme hupendelea mtu asemaye kwa unyofu;

humpenda mtu asemaye ukweli.

14Hasira ya mfalme ni kama mjumbe wa kifo;

mtu mwenye busara ataituliza.

15Uso wa mfalme ukingaa kuna uhai;

wema wake ni kama wingu la masika.

16Kupata hekima ni bora kuliko dhahabu;

kupata akili ni chaguo bora kuliko fedha.

17Njia ya wanyofu huepukana na uovu;

anayechunga njia yake huhifadhi maisha yake.

18Kiburi hutangulia maangamizi;

majivuno hutangulia maanguko.

19Afadhali kuwa mnyenyekevu na kuwa maskini,

kuliko kugawana nyara na wenye kiburi.

20Anayezingatia mafundisho atafanikiwa;

heri mtu yule anayemtumainia Mwenyezi-Mungu.

21Mwenye hekima moyoni huitwa mwenye akili;

neno la kupendeza huwavutia watu.

22Hekima ni chemchemi ya uhai kwake aliye nayo,

bali upumbavu ni adhabu ya wapumbavu.

23Moyo wa mwenye hekima humwezesha kusema kwa busara;

huyafanya maneno yake yawe ya kuvutia.

24Maneno mazuri ni kama asali;

ni matamu rohoni na yenye kuupa mwili afya.

25Mtu aweza kuona njia yake kuwa sawa,[#Taz Meth 14:12]

lakini mwishowe humwongoza kwenye kifo.

26Hamu ya chakula humhimiza mfanyakazi,

maana njaa yake humsukuma aendelee.

27Mtu mwovu hupanga uovu;

maneno yake ni kama moto mkali.

28Mtu mpotovu hueneza ugomvi,

mfitini hutenganisha marafiki.

29Mtu mkatili humshawishi jirani yake;

humwongoza katika njia mbaya.

30Anayekonyeza jicho kwa hila amepanga maovu;

anayekaza midomo amekwisha nuia mabaya.

31Kuwa na mvi za uzee ni taji la utukufu;

hupatikana kwa maisha ya uadilifu.

32Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwenye nguvu;

aitawalaye nafsi yake ni bora kuliko autekaye mji.

33Kura hupigwa kujua yatakayotukia,

lakini uamuzi ni wake Mwenyezi-Mungu.

Swahili Common Language DC Bible: Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki © Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya, 1995, 2001. Haki zote zimehifadhiwa.  
Published by: Bible Society of Tanzania