2 Mambo 7

Kuumaliza mweuo wa Nyumba ya Mungu.

1Salomo alipokwisha kuomba, ndipo, moto uliposhuka toka mbinguni, ukala ng'ombe ya tambiko ya kuteketezwa nzima na ng'ombe nyingine za tambiko, kisha utukufu wa Bwana ukajaa mle Nyumbani.[#2 Mose 40:34; 3 Mose 9:24; 1 Fal. 18:38.]

2Kwa hiyo watambikaji hawakuweza kuingia Nyumbani mwa Bwana, kwa kuwa utukufu wa Bwana ulijaa Nyumbani mwa Bwana.

3Nao wana wote wa Isiraeli walipoona, jinsi moto ulivyoshuka nao utukufu wa Bwana ulivyokaa juu ya Nyumba hii, wakapiga magoti na kujinamisha chini hapo palipopigiliwa mawe, wakamwangukia Bwana na kumshukuru, ya kuwa ni mwema, ya kuwa upole wake ni wa kale na kale.[#2 Mambo 5:13; Sh. 136.]

(4-10: 1 Fal. 8:62-66.)

4Kisha mfalme na mkutano wote wa watu wakamtolea Bwana ng'ombe za tambiko.

5Mfalme Salomo akatoa ng'ombe 22000 na mbuzi na kondoo 120000 kuwa ng'ombe za tambiko. Ndivyo, mfalme na watu wote walivyoieua Nyumba ya Mungu.

6Watambikaji wakawa wakisimama na kuziangalia kazi zao, nao Walawi wakashika vyombo vya kumwimbia Bwana, mfalme Dawidi alivyovitengeneza hapo, alipomshangilia Bwana, navyo vikamshukuru Bwana kwamba: Upole wake ni wa kale na kale; nao watambikaji waliowaelekea wakapiga matarumbeta, nao Waisiraeli wote walikuwa wamesimama.

7Ndipo, Salomo alipokitakasa kipande cha kati cha ua uliokuwa mbele ya Nyumba ya Bwana, kwani ndiko, alikotolea ng'ombe za tambiko za kuteketezwa nzima na mafuta ya ng'ombe za tambiko za shukrani, kwani ile meza ya shaba ya kutambikia, Salomo aliyoitengeneza, haikuweza kuzieneza ng'ombe za tambiko za kuteketezwa nzima na vilaji vya tambiko na mafuta ya ng'ombe nyingine za tambiko.

8Ndivyo, Salomo alivyofanya wakati huo sikukuu ya siku saba, yeye pamoja nao Waisiraeli wote, wakawa mkutano mkubwa sana wa watu waliotoka Hamati mpaka kwenye mto wa Misri.

9Siku ya nane wakakusanyika tena kufanya sikukuu; kwani zile siku saba ndizo, walizoieneza meza ya kutambikia ng'ombe za tambiko, hii sikukuu nayo ikawa ya siku saba tena.[#4 Mose 7:10.]

10Siku ya ishirini na tatu ya mwezi wa saba akawapa watu ruhusa kwenda mahemani kwao, wakifurahi na kuchangamka mioyoni kwa wema, Bwana aliomfanyizia Dawidi naye Salomo nao walio ukoo wake wa Waisiraeli.

Mungu anamtokea Salomo mara ya pili.

(11-22: 1 Fal. 9:1-9.)

11Salomo alipoimaliza Nyumba ya Bwana na nyumba ya mfalme na kufanikiwa yote, yeye Salomo aliyokuwa nayo moyoni ya kufanya Nyumbani mwa Bwana namo nyumbani mwake,

12ndipo, Bwana alipomtokea Salomo usiku, akamwambia: Nimeyasikia maombo yako, napo mahali hapa nimepachagua, pawe Nyumba ya kunitambikia.[#5 Mose 12:5.]

13Itakuwa, nizizibe mbingu, mvua isinye, au niagize nzige, waile nchi hii, au nitume magonjwa mabaya kwao walio ukoo wangu,

14basi, wao walio ukoo wangu, walioitwa kwa Jina langu, watakaponyenyekea na kuniomba wakiutafuta uso wangu, warudi na kuziacha njia zao mbaya, ndipo, nitakapowasikia huko mbinguni, niwaondolee makosa yao, niiponye hii nchi yao.

15Tangu sasa macho yangu yatakuwa wazi, nayo masikio yangu yatakuwa yametegwa kuyasikiliza, watakayoniomba mahali hapa.[#2 Mambo 6:40.]

16Sasa nimeichagua Nyumba hii, nikaitakasa, Jina langu lipate kuwa humu kale na kale, nayo macho yangu na moyo wangu yatakuwa humu siku zote.

17Wewe nawe ukiendelea kuwa machoni pangu, kama baba yako Dawidi alivyoendelea, uyafanye yote, niliyokuagiza, ukiyaangalia maongozi yangu na maamuzi yangu,

18ndipo, nitakapokisimamisha kiti cha kifalme cha ufalme wako, kama nilivyomwagia baba yako Dawidi kwamba: Kwako hakutakoseka mtu atakayewatawala Waisiraeli.[#2 Sam. 7:12,16.]

19Lakini ninyi mtakaporudi nyuma, myaache maagizo yangu na maongozi yangu, niliyoyatoa machoni penu, mkaja kutumikia miungu mingine na kuiangukia,

20ndipo, nitakapowang'oa katika hii nchi yangu, niliyowapa, nayo Nyumba hii, niliyoitakasa kuwa Kao la Jina langu, nitaitupa, macho yangu yasiione tena, nitaitoa kuwa fumbo na simango kwa makabila yote.[#5 Mose 28:37.]

21Nayo Nyumba hii iliyokuwa imetukuka kabisa, basi, kila atakayepita hapo ataistukia na kuuliza: Kwa sababu gani Bwana ameifanyizia hivi nchi hii na Nyumba hii?[#5 Mose 29:24-27; Yer. 22:8-9.]

22Ndipo, watakapojibu: Kwa kuwa walimwacha Bwana Mungu wa baba zao aliyewatoa katika nchi ya Misri, wakashikamana na miungu mingine, wakaiangukia na kuitumikia, hii ndiyo sababu, akiwaletea haya mabaya yote.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania