Hosea 12

Hosea 12

Baba Yakobo ni kielezo chao Waisiraeli.

1Efuraimu amenizingia uwongo,

walio mlango wa Isiraeli wamenizingia udanganyifu;

Yuda naye hata sasa hujiendea na kumwacha Mungu

aliye mtakatifu na mwelekevu.

2Efuraimu hujilisha upepo,

huukimbilia upepo utokao maawioni kwa jua,

siku kwa siku huongeza uwongo na uangamizo:

hufanya maagano na Asuri, tena mafuta hupelekwa Misri.

3Lakini Bwana yuko na shauri na Yuda, ampatilizie Yakobo njia zake

na kumlipisha matendo yake.

4Tumboni mwa mama alimshika kaka yake kisigino,

napo, alipokuwa mtu mzima, alishindana na Mungu.

5Akashindana na malaika, akamshinda kwa kulia na kumlalamikia;

Beteli ndiko, alikomwona, ndiko, alikosema na sisi

6yeye Bwana Mungu Mwenye vikosi; Bwana ni Jina lake la kumtukuza.[#Sh. 83:18.]

7Nawe sharti urudi kwa Mungu wako, ushikamane na upole,

ufanye yapasayo, umngojee Mungu wako pasipo kukoma.

8Kwa kushika mizani ya kudanganyia mikononi mwake

Mkanaani hupenda kukorofisha.

9Efuraimu husema: Kumbe ni tajiri! Nimejipatia mali!

Tena kwa hivyo vyote, nilivyovisumbukia,

hawataniona, ya kuwa nimefanya kiovu cha kumkosea mtu.

10Lakini mimi Bwana ni Mungu wako

tangu hapo, nilipokutoa katika nchi ya Misri,

mimi nitakukalisha tena katika mahema kama penye sikukuu za mkutano.

11Mimi nilisema na wafumbuaji, nikawatokea mara nyingi,

nikawaonya kwa vinywa vya wafumbuaji na kusema mifano.

12Kwa kuwa huko Gileadi walifanya yasiyofaa,

basi, nao watageuzwa kuwa si kitu;

kwa kuwa huko Gilgali walitoa ng'ombe za tambiko,

napo pao pa kutambikia patakuwa kama chungu za mawe penye matuta.

13Yakobo alikimbilia mashamba ya Aramu,

Isiraeli akatumikia kupata mwanamke,

hakuwa na budi kuchunga kondoo na mbuzi, ampate mkewe.

14Lakini kwa mkono wa mfumbuaji Bwana alimtoa Isiraeli huko

Misri,

kisha wakachungwa na mfumbuaji.

15Efuraimu amemsikitisha masikitiko yenye uchungu;

kwa hiyo zile damu, alizozimwaga, atamtupia, zimkalie,

nayo matusi yake ndiyo, Bwana wake atakayomlipisha.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania