2 Samweli 21

2 Samweli 21

Daudi ajilipiza kwa Wagibeoni

1Kulikuwa na njaa siku za Daudi muda wa miaka mitatu, mwaka kwa mwaka; naye Daudi akautafuta uso wa BWANA. BWANA akasema, Ni kwa ajili ya Sauli, na kwa nyumba yake yenye damu, kwa kuwa aliwaua hao Wagibeoni.[#Hes 27:21; 1 Sam 22:10-15; Law 18:25; Hes 35:33; Isa 26:21]

2Ndipo mfalme akawaita Wagibeoni akawaambia; (basi Wagibeoni si wa wana wa Israeli, ila ni wa masalio ya Waamori; na wana wa Israeli walikuwa wamewaapia; lakini Sauli akajaribu kuwaua kwa ari kwa ajili ya wana wa Israeli na Yuda;)[#Yos 9:3-15]

3basi Daudi akawaambia hao Wagibeoni, Niwatendee nini? Na kwa tendo gani nifanye upatanisho, mpate kuubariki urithi wa BWANA?[#2 Sam 20:19]

4Na hao Wagibeoni wakamwambia, Si jambo la fedha wala dhahabu lililo kati ya sisi na Sauli, au nyumba yake; wala si juu yetu kumwua mtu yeyote katika Israeli. Akasema, Mtakayonena, ndiyo nitakayowatendea ninyi.

5Wakamwambia mfalme, Yule mtu aliyetupoteza, na kutufanyia shauri la kutuharibu, tusikae katika mipaka yoyote ya Israeli,

6basi, na tutolewe watu saba katika wanawe, nasi tutawatundika mbele za BWANA katika Gibeoni, katika mlima wa BWANA. Mfalme akasema, Nitawatoa.[#Amu 20:4; 1 Sam 10:24,26]

7Lakini mfalme akamwachilia Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli, kwa ajili ya kiapo cha BWANA kilichokuwa kati yao, yaani, kati ya Daudi na Yonathani, mwana wa Sauli.[#1 Sam 20:8,15-17,42; 23:18; 18:3; 2 Sam 9:1-7]

8Ila mfalme akawatwaa hao wana wawili wa Rispa, binti Aya, aliomzalia Sauli, Armoni na Mefiboshethi; na wana watano wa Merabu binti Sauli, aliomzalia Adrieli, mwana wa Barzilai, Mmeholathi;[#1 Sam 18:19; 2 Sam 3:7]

9akawatia mikononi mwa Wagibeoni, nao wakawatundika mlimani mbele za BWANA, nao wakaangamia wote saba pamoja; wakauawa siku za mavuno, za kwanza, mwanzo wa mavuno ya shayiri.[#2 Sam 6:17]

10Naye Rispa, binti Aya, akatwaa nguo ya magunia akajitandikia mwambani, tangu mwanzo wa mavuno hadi waliponyeshewa mvua toka mbinguni; wala hakuacha ndege wa angani kukaa juu yao mchana, wala wanyama wa mwitu usiku.[#2 Sam 3:7; Kum 21:23]

11Kisha Daudi akaambiwa hayo aliyoyafanya huyo Rispa binti Aya, suria wa Sauli.

12Akaenda Daudi, akaitwaa mifupa ya Sauli na mifupa ya Yonathani mwanawe mikononi mwa watu wa Yabesh-gileadi; waliyoiiba katika njia ya Beth-sheani, hapo Wafilisti walipowatungika, katika siku hiyo waliyomwua Sauli huko Gilboa;[#1 Sam 31:8-13]

13naye akaileta toka huko hiyo mifupa ya Sauli, na mifupa ya Yonathani mwanawe; nao wakaizoa mifupa yao waliotundikwa.

14Kisha wakaizika mifupa ya Sauli na ya Yonathani mwanawe katika nchi ya Benyamini, huko Zela, kaburini mwa Kishi babaye; wakafanya yote aliyoyaamuru mfalme. Na baadaye Mungu aliiridhia hiyo nchi.[#Yos 18:28; 7:26; 2 Sam 24:25]

Ushujaa wa jeshi la Daudi

15Basi kulikuwa na vita tena kati ya Wafilisti na Israeli; Daudi akashuka mpaka Gobu, na watumishi wake pamoja naye, akapigana na Wafilisti; naye Daudi akaishiwa na nguvu.

16Naye Ishi-benobu, aliyekuwa mmoja wa Warefai, ambaye uzito wa mkuki wake ulikuwa shekeli mia tatu za shaba kwa uzani, naye amejifungia upanga mpya, alijaribu kumwua Daudi.[#21:16 Au, wana wa majitu.]

17Lakini Abishai, mwana wa Seruya, akamsaidia, akampiga Mfilisti, akamwua. Ndipo watu wa Daudi wakamwapia, wakasema, Wewe hutatoka tena pamoja nasi kwenda vitani, usije ukaizima taa ya Israeli.[#1 Fal 11:36; Zab 132:17]

18Ikawa baada ya hayo, kulikuwa na vita tena na Wafilisti huko Gobu; ndipo Sibekai, Mhushathi, alipomwua Safu, aliyekuwa mmoja wa Warefai.[#1 Nya 11:29]

19Kulikuwa na vita tena na Wafilisti huko Gobu; na Elhanani, mwana wa Yairi, Mbethlehemi, alimwua Goliathi, Mgiti, ambaye mpini wa mkuki wake ulikuwa kama mpini wa mfuma nguo

20Kulikuwa na vita tena huko Gathi; ambako kulikuwa na mtu mrefu sana, mwenye vidole sita katika kila mkono, na vidole sita katika kila mguu, jumla yake ishirini na vinne; yeye naye alizaliwa kwa Mrefai.[#1 Nya 20:6]

21Naye huyo alipowatukana Israeli, ndipo Yonathani, mwana wa Shimei, nduguye Daudi, akamwua.

22Hao wanne walizaliwa kwake huyo Mrefai wa Gathi; wakaanguka kwa mkono wa Daudi, na kwa mikono ya watumishi wake.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya