Zaburi 2

Zaburi 2

Mfalme mteule wa Mungu

1Kwa nini mataifa yanafanya ghasia?[#Taz Mate 4:25-26]

Mbona watu wanafanya njama za bure?

2Wafalme wa dunia wanajitayarisha;

watawala wanashauriana pamoja,

dhidi ya Mwenyezi-Mungu na mteule wake.

3Wanasema: “Tujiondoe katika utawala wao;

tutupilie mbali minyororo yao!”

4Mwenyezi-Mungu atawalaye juu mbinguni,

anawacheka na kuwadhihaki.

5Kisha, anawakaripia kwa ghadhabu,

na kuwatisha kwa hasira, akisema:

6“Nimemtawaza mfalme niliyemteua,

anatawala Siyoni, mlima wangu mtakatifu!”

7Mfalme asema: “Nitatangaza azimio la Mwenyezi-Mungu.[#Taz Mate 13:33; Ebr 1:5; 5:5; #2:7 Kwanza wafalme wanasema (aya ya 3), pili Mwenyezi-Mungu anasema (aya ya 6), tatu mfalme mteule anasema (aya ya 7).]

Mungu aliniambia:

‘Wewe ni mwanangu,

mimi leo nimekuwa baba yako.

8Niombe nami nitakupa mataifa yawe urithi wako,

na dunia nzima kuwa mali yako.

9Utawaponda kwa fimbo ya chuma;[#Taz Ufu 2:26,27; 12:5; 19:15]

utawavunja kama chungu cha mfinyanzi!’”

10Sasa enyi wafalme, tumieni busara;

sikilizeni onyo hili, enyi watawala wa dunia.

11Mtumikieni Mwenyezi-Mungu kwa uchaji;

12msujudieni na kutetemeka;[#2:12 Kiebrania: Mbusuni mwana kwa kutetemeka. Lakini maana yake si dhahiri.]

asije akakasirika, mkaangamia ghafla;

kwani hasira yake huwaka haraka.

Heri yao wote wanaokimbilia usalama kwake!

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania