Zaburi 86

Zaburi 86

Kuomba msaada

1Unitegee sikio, ee Mwenyezi-Mungu, unijibu,

maana mimi ni fukara na mnyonge.

2Uyahifadhi maisha yangu maana mimi ni mchaji wako;

uniokoe mimi mtumishi wako ninayekutegemea.

3Wewe ni Mungu wangu;

basi, unionee huruma,

maana nakulilia mchana kutwa.

4Uifurahishe roho yangu mimi mtumishi wako,

maana sala zangu nazielekeza kwako ee Bwana.

5Wewe, ee Bwana, u mwema na mwenye kusamehe;

mwingi wa fadhili kwa wote wakuombao.

6Ee Mwenyezi-Mungu, uitegee sikio sala yangu;

ukisikie kilio cha ombi langu.

7Siku za taabu nakuita,

maana wewe waniitikia.

8Ee Bwana, hakuna Mungu aliye kama wewe;

hakuna awezaye kufanya unayofanya wewe.

9Mataifa yote uliyoyaumba, yatakuja kukuabudu, ee Bwana;[#Taz Ufu 15:4]

yatatangaza ukuu wa jina lako.

10Wewe ndiwe mkuu, wafanya maajabu;

wewe peke yako ndiwe Mungu.

11Unifundishe njia yako, ee Mwenyezi-Mungu,

nipate kuwa mwaminifu kwako;

uongoze moyo wangu nikuheshimu.

12Ee Bwana, Mungu wangu, nitakusifu kwa moyo wote;

nitatangaza ukuu wa jina lako milele.

13Fadhili zako kwangu ni nyingi mno!

Umeniokoa kutoka chini kuzimu.

14Ee Mungu, watu wenye kiburi wamenikabili;

kundi la watu wakatili wanataka kuniua,

wala hawakujali wewe hata kidogo.

15Lakini wewe Bwana, ni Mungu wa rehema na huruma;

wewe ni mvumilivu, mwingi wa fadhili na uaminifu.

16Unigeukie, unihurumie;

unijalie nguvu yako mimi mtumishi wako,

umwokoe mtoto wa mjakazi wako.

17Unioneshe ishara ya wema wako, ee Mwenyezi-Mungu,

ili wale wanaonichukia waaibike,

waonapo umenisaidia na kunifariji.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania