Wimbo Ulio Bora 6

Wimbo Ulio Bora 6

Wanawake

1Ewe mwanamke uliye mzuri sana;

amekwenda wapi huyo mpenzi wako?

Ameelekea wapi mpenzi wako

ili tupate kushirikiana nawe katika kumtafuta?

Bibi arusi

2Mpenzi wangu amekwenda bustanini mwake,

mahali ambapo rihani hustawi.

Yeye analisha kondoo wake

na kukusanya yungiyungi.

3Mimi ni wake mpenzi wangu, naye ni wangu;

yeye huwalisha kondoo wake penye yungiyungi.

Shairi la tano

Bwana arusi

4Mpenzi wangu, wewe u mzuri kama Tirza,

wapendeza kama Yerusalemu,

unatisha kama jeshi lenye bendera.

5Hebu tazama kando tafadhali;

ukinitazama nahangaika.

Nywele zako ni kama kundi la mbuzi,

wateremkao chini ya milima ya Gileadi.

6Meno yako kama kundi la kondoo majike

wanaoteremka baada ya kuogeshwa.

Kila mmoja amezaa mapacha,

na hakuna yeyote aliyefiwa.

7Mashavu yako ni kama nusu mbili za komamanga,

nyuma ya shela lako.

8Wapo malkia sitini, masuria themanini,

na wasichana wasiohesabika!

9Hua wangu, mzuri wangu, ni mmoja tu,

na ni kipenzi cha mama yake;

yeye ni wa pekee kwa mama yake.

Wasichana humtazama na kumwita heri,

nao malkia na masuria huziimba sifa zake.

10Nani huyu atazamaye kama pambazuko?

Mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua,

na anatisha kama jeshi lenye bendera.

11Nimeingia katika bustani ya milozi

kutazama machipuko ya bondeni,

kuona kama mizabibu imechanua,

na mikomamanga imechanua maua.

12Bila kutazamia, mpenzi wangu,

akanitia katika gari la mkuu.

Wanawake

13Rudi, rudi ewe msichana wa Mshulami.

Rudi, rudi tupate kukutazama.

Bibi arusi

Mbona mwataka kunitazama miye Mshulami

kana kwamba mnatazama ngoma

kati ya majeshi mawili?

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania