The chat will start when you send the first message.
1Ewe mwanamke uliye mzuri sana;
amekwenda wapi huyo mpenzi wako?
Ameelekea wapi mpenzi wako
ili tupate kushirikiana nawe katika kumtafuta?
2Mpenzi wangu amekwenda bustanini mwake,
mahali ambapo rihani hustawi.
Yeye analisha kondoo wake
na kukusanya yungiyungi.
3Mimi ni wake mpenzi wangu, naye ni wangu;
yeye huwalisha kondoo wake penye yungiyungi.
4Mpenzi wangu, wewe u mzuri kama Tirza,
wapendeza kama Yerusalemu,
unatisha kama jeshi lenye bendera.
5Hebu tazama kando tafadhali;
ukinitazama nahangaika.
Nywele zako ni kama kundi la mbuzi,
wateremkao chini ya milima ya Gileadi.
6Meno yako kama kundi la kondoo majike
wanaoteremka baada ya kuogeshwa.
Kila mmoja amezaa mapacha,
na hakuna yeyote aliyefiwa.
7Mashavu yako ni kama nusu mbili za komamanga,
nyuma ya shela lako.
8Wapo malkia sitini, masuria themanini,
na wasichana wasiohesabika!
9Hua wangu, mzuri wangu, ni mmoja tu,
na ni kipenzi cha mama yake;
yeye ni wa pekee kwa mama yake.
Wasichana humtazama na kumwita heri,
nao malkia na masuria huziimba sifa zake.
10Nani huyu atazamaye kama pambazuko?
Mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua,
na anatisha kama jeshi lenye bendera.
11Nimeingia katika bustani ya milozi
kutazama machipuko ya bondeni,
kuona kama mizabibu imechanua,
na mikomamanga imechanua maua.
12Bila kutazamia, mpenzi wangu,
akanitia katika gari la mkuu.
13Rudi, rudi ewe msichana wa Mshulami.
Rudi, rudi tupate kukutazama.
Mbona mwataka kunitazama miye Mshulami
kana kwamba mnatazama ngoma
kati ya majeshi mawili?