Wimbo Ulio Bora 8

Wimbo Ulio Bora 8

1Laiti ungekuwa kaka yangu,

ambaye amenyonyeshwa na mama yangu!

Hivyo, hata kama ningekutana nawe nje,

ningekubusu na hakuna ambaye angenidharau.

2Ningekuongoza na kukufikisha nyumbani kwa mama mzazi,

mahali ambapo ungenifundisha upendo.

Ningekupa divai nzuri iliyokolezwa,

ningekupa divai yangu ya makomamanga yangu.

3Mkono wako wa kushoto u chini ya kichwa changu,

na mkono wako wa kulia wanikumbatia.

4Nawasihini, enyi wanawake wa Yerusalemu,

msiyachochee wala kuyaamsha mapenzi,

hadi hapo wakati wake utakapofika.

Shairi la sita

Wanawake

5Ni nani huyu ajaye kutoka mbugani,

huku anamwegemea mpenzi wake?

Bibi arusi

Chini ya mtofaa, mimi nilikuamsha,

pale ambapo mama yako aliona uchungu,

naam, pale ambapo mama yako alikuzaa.

6Nipige kama mhuri moyoni mwako,

naam, kama mhuri mikononi mwako.

Maana pendo lina nguvu kama kifo,

wivu nao ni mkatili kama kaburi.

Mlipuko wake ni kama mlipuko wa moto,

huwaka kama mwali wa moto.

7Maji mengi hayawezi kamwe kulizima,

mafuriko hayawezi kulizamisha.

Mtu akijaribu kununua pendo,

akalitolea mali yake yote,

atakachopata ni dharau tupu.

Ndugu za Bibi arusi

8Tunaye dada mdogo,

ambaye bado hajaota matiti.

Je, tumfanyie nini dada yetu

siku atakapoposwa?

9Kama angalikuwa ukuta,

tungalimjengea mnara wa fedha;

na kama angalikuwa mlango,

tungalimhifadhi kwa mbao za mierezi.

Bibi arusi

10Mimi nalikuwa ukuta,

na matiti yangu kama minara yake.

Machoni pake nalikuwa

kama mwenye kuleta amani.

Bwana arusi

11Solomoni alikuwa ana shamba la mizabibu,

mahali paitwapo Baal-hamoni.

Alilikodisha kwa walinzi;

kila mmoja wao alilipa vipande elfu vya fedha.

12Shamba langu la mizabibu ni shamba langu mwenyewe,

naam, ni shamba langu binafsi!

Basi, Solomoni, wewe ukae na elfu zako za fedha,

na kila mlinzi wa matunda akae na mia mbili zake.

13Ewe uliye shambani,

rafiki zangu wanasikiliza sauti yako;

hebu nami niisikie tafadhali!

Bibi arusi

14Njoo haraka ewe mpenzi wangu,

kama paa au mwanapaa dume juu ya milima ya manukato.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania