Methali 20

Methali 20

1Divai huleta dhihaka na kileo huleta ugomvi;

yeyote anayevutiwa navyo hana hekima.

2Ghadhabu kali ya mfalme ni kama simba angurumaye;[#20:2 Si dhahiri kama msemo huu unasema hivyo kwa jumla bila kugusia kwamba ni hasira halali au la. Katika 19:12; 20:8,26,28 inahusu mfalme aliye mwema.]

anayemkasirisha anayahatarisha maisha yake.

3Ni jambo la heshima kuepa ugomvi;

wapumbavu ndio wanaogombana.

4Mvivu halimi wakati wa kulima;

wakati wa mavuno atatafuta asipate chochote.

5Fikira za mtu zimefichika kama kilindi cha maji;

lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.

6Watu wengi hujivunia kuwa wema,

lakini mwaminifu wa kweli apatikana wapi?

7Mtu mwadilifu akiishi kwa unyofu;

watoto wake atakaowaacha watabarikiwa.

8Mfalme mwema aketipo kutoa hukumu,

huupepeta uovu wote kwa macho yake.

9Nani athubutuye kusema: “Nimeutakasa moyo wangu;

mimi nimetakasika dhambi yangu?”

10Mizani ya udanganyifu na vipimo vya udanganyifu,

vyote ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu.

11Hata mtoto hujulikana kwa matendo yake,

kama tabia yake ni njema na aminifu.

12Sikio lisikialo na jicho lionalo,

yote mawili kayafanya Mwenyezi-Mungu.

13Usipende kulala tu usije ukawa maskini;

uwe macho nawe utakuwa na chakula kingi.

14“Hakifai, hakifai”, mnunuzi hulalamika,

lakini akiondoka hujisifu amepunguziwa bei.

15Kuna dhahabu na wingi wa mawe ya thamani kubwa;

lakini cha thamani kubwa zaidi ni maneno ya busara!

16Mtu akiahidi mbele yako kumdhamini mgeni,

chukua nguo yake;

mfanye awajibike kwa kuwadhamini wageni.

17Chakula kipatikanacho kwa udanganyifu ni kitamu,

lakini baadaye huwa kama mchanga kinywani.

18Mipango mizuri hufanyika kwa kushauriana;

ukitaka kuanza vita lazima kutafakari kwanza.

19Mpiga domo hafichi siri,

kwa hiyo mwepe mtu wa kuropoka.

20Anayemlaani baba yake au mama yake,[#20:20 Taz 10:13; 14:3; 19:29.]

mwanga wa uhai wake utazimwa kama taa gizani.

21Mali iliyopatikana kwa haraka mwanzoni,

haitakuwa ya heri mwishoni.

22Usiseme, “Nitalipiza ubaya niliotendewa.”

Mtegemee Mwenyezi-Mungu naye atakusaidia.

23Mizani ya udanganyifu ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu,

na vipimo visivyo halali ni kitu kibaya.

24Hatua za mtu huongozwa na Mwenyezi-Mungu;

awezaje binadamu kujua njia ya kwenda?

25Ni hatari kusema kwa mzaha “Usiahidi kumpa Mungu kitu bila kufikiri,

la sivyo utaanza kusikitika baada ya nadhiri yako.”

26Mfalme mwenye busara huwapepeta waovu;

huwaadhibu bila huruma.

27Dhamiri ya mtu ni taa ya Mwenyezi-Mungu;

huchunguza nafsi yake mtu mpaka ndani kabisa.

28Wema na uaminifu humkinga mfalme;

utawala wake huimarishwa kwa uadilifu.

29Fahari ya vijana ni nguvu zao,

uzuri wa vikongwe ni mvi za uzee.

30Mapigo yanayoumiza ni dawa ya kuondoa uovu;

viboko husafisha nafsi mpaka ndani kabisa.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania