Zaburi 102

Zaburi 102

Sala katika taabu

1Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu,

na kilio changu kikufikie.

2Usijifiche mbali nami wakati wa taabu!

Unitegee sikio lako,

unijibu upesi wakati ninapokuomba!

3Siku zangu zapita kama moshi;

mifupa yangu yaungua kama katika tanuri.

4Nimepondwa moyoni kama nyasi na kunyauka;

sina hata hamu ya chakula.

5Kutokana na kusononeka kwangu,

nimebaki mifupa na ngozi.

6Nimekuwa kama ndege wa jangwani;

kama bundi kwenye mahame.

7Ninalala macho wazi,

kama ndege mkiwa juu ya paa.

8Mchana kutwa maadui zangu wananisimanga,

wanaonidhihaki hutumia jina langu kulaania.

9Majivu yamekuwa chakula changu,[#102:9 Katika Biblia mara nyingi “majivu” yanatumika kama mfano wa maombolezo na huzuni na kwa sababu hiyo mstari huu wa kwanza wa aya hii ni sambamba kimaana na mstari wa pili.]

machozi nayachanganya na kinywaji changu,

10kwa sababu ya ghadhabu na hasira yako,

maana umeniokota na kunitupilia mbali.

11Maisha yangu ni kama kivuli cha jioni;

ninanyauka kama nyasi.

12Lakini wewe, ee Mwenyezi-Mungu, watawala milele;

jina lako lakumbukwa vizazi vyote.

13Wewe utainuka na kuurehemu mji wa Siyoni;

maana wakati umefika wa kuutendea mema;

wakati wake uliopangwa umefika.

14Watumishi wako wanauthamini sana,

ujapokuwa magofu sasa;

wanauonea huruma,

ingawa umeharibika kabisa.

15Mataifa yataliheshimu jina la Mwenyezi-Mungu;

wafalme wote duniani wataogopa utukufu wake.

16Mwenyezi-Mungu ataijenga upya Siyoni,

na kuonekana alivyo mtukufu.

17Ataikubali sala ya fukara;

wala hatayakataa maombi yao.

18Andika jambo hili kwa ajili ya vizazi vijavyo;

watakaozaliwa baadaye wamsifu Mwenyezi-Mungu.

19Kwamba aliangalia chini kutoka patakatifu pake juu,

Mwenyezi-Mungu aliangalia dunia kutoka mbinguni,

20akasikia lalamiko la wafungwa;[#102:20 Labda hapa “wafungwa” ni wale watu waliopelekwa uhamishoni na ambao katika aya 17 wanaitwa fukara yaani wasio na kitu na labda bila makao.]

akawaachilia huru waliohukumiwa kuuawa.

21Hivyo watu watatangaza jina la Mwenyezi-Mungu huko Siyoni;

sifa zake zitatangazwa huko Yerusalemu,

22wakati mataifa yatakapokusanyika pamoja

na falme zitakutana kumwabudu Mwenyezi-Mungu.

23Mungu amenipunguzia nguvu ningali kijana;

ameyafupisha maisha yangu.

24Ee Mungu wangu, usinichukue sasa

wakati ningali bado kijana.

Ee Mwenyezi-Mungu wewe wadumu milele.

25Wewe uliiumba dunia zamani za kale,[#102:25 Hapa Mwanazaburi anakumbusha kwa kifupi simulizi lile refu la kuumbwa ulimwengu katika Mwa 1:3-10.]

mbingu ni kazi ya mikono yako.

26Hizo zitatoweka, lakini wewe wabaki;

hizo zitachakaa kama vazi.

Utazitupilia mbali kama nguo,

nazo zitapotelea mbali.

27Lakini wewe ni yuleyule daima,

na maisha yako hayana mwisho.

28Watoto wa watumishi wako watakaa salama;

wazawa wao wataimarishwa mbele yako.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania