Zaburi 58

Zaburi 58

Mungu hakimu wa mahakimu

1Enyi watawala, je, mwahukumu kwa haki kweli?

Je, mnawahukumu watu kwa adili?

2La! Nyinyi mwafikiria tu kutenda maovu;

nyinyi wenyewe mwaeneza dhuluma nchini.

3Waovu wamepotoka tangu kuzaliwa kwao,

waongo hao, wamekosa tangu walipozaliwa.

4Wana sumu kama sumu ya nyoka;[#58:4-5 Huyu Mwanazaburi anafananisha watawala wabaya na nyoka. “Viziwi”, yaani hawawezi kusikia maonyo. Picha inayotolewa katika aya 4b-5 si rahisi kuielewa na wengi hutoa tafsiri tofauti tofauti. Lakini maana ya kawaida ni kwamba watawala hao ni wakaidi, hukataa kusikiliza mashauri mema.]

viziwi kama joka lizibalo masikio,

5ambalo halisikii hata sauti ya mlozi,

au utenzi wa mganga stadi wa uchawi.

6Ee Mungu, wavunje meno yao,

yang'oe, ee Mwenyezi-Mungu, meno ya simba hao.

7Watoweke kama maji yanayodidimia mchangani,

kama nyasi wakanyagwe na kunyauka,

8watoweke kama konokono ayeyukavyo,[#58:8 Ilifikiriwa kwamba konokono anapoacha ute wa mwili wake nyuma anapojikokota, alikuwa anayeyuka na mwishowe ataishia kabisa. Ndivyo watakavyoishia hao watu wabaya.]

kama mimba iliyoharibika isiyoona kamwe jua!

9Kabla hawajatambua, wang'olewe

kama miiba, michongoma au magugu.

Kwa hasira ya Mungu, wapeperushwe mbali,

wakiwa bado hai.

10Waadilifu watafurahi waonapo waovu wanaadhibiwa;

watatembea katika damu ya watu wabaya.

11Watu wote watasema: “Naam, waadilifu hupata tuzo!

Hakika yuko Mungu anayeihukumu dunia!”

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania