Zaburi 97

Zaburi 97

Mungu mtawala mkuu

1Mwenyezi-Mungu anatawala!

Furahi, ee dunia!

Furahini enyi visiwa vingi!

2Mawingu na giza nene vyamzunguka;

uadilifu na haki ni msingi wa utawala wake.

3Moto watangulia mbele yake,

na kuwateketeza maadui zake pande zote.

4Umeme wake wauangaza ulimwengu;

dunia yauona na kutetemeka.

5Milima yayeyuka kama nta mbele ya Mwenyezi-Mungu;[#97:2-5 Mwanazaburi, kwa ukamilifu kabisa anatumia picha zote za Biblia ambazo zinatumiwa mara nyingi kueleza kuweko au kutokea kwake Mwenyezi-Mungu. Kwa kuwa yeye ni mfalme mkuu na Muumba wa vyote, viumbe vyote na hata visivyo na uhai vinaguswa na hivyo kuonesha uwezo wake mkuu. Taz 18:7-15; 29:3-9; 46:6-7; 83:13-16.]

naam, mbele ya Bwana wa dunia yote.

6Mbingu zatangaza uadilifu wake;

na mataifa yote yauona utukufu wake.

7Wote wanaoabudu sanamu wanaaibishwa,

naam, wote wanaojisifia miungu duni;

miungu yote husujudu mbele zake.

8Watu wa Siyoni wanafurahi;

watu wa Yuda wanashangilia,

kwa sababu ya hukumu zako, ee Mungu.

9Wewe Mwenyezi-Mungu ni mkuu juu ya dunia yote;

wewe watukuka juu ya miungu yote.

10Mwenyezi-Mungu huwapenda wanaochukia uovu,

huyalinda maisha ya watu wake;

huwaokoa makuchani mwa waovu.

11Mwanga humwangazia mtu mwadilifu,[#97:11 Mwanga ni mfano au kielelezo cha wokovu wa Mungu; ni picha ya fadhili na baraka za Mungu ambazo zinamiminiwa watu wake.]

na furaha kwa watu wanyofu wa moyo.

12Furahini kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu;

mshukuruni kwa ajili ya jina lake takatifu.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania