The chat will start when you send the first message.
1Kutoka kwangu mimi Paulo, mtumishi wa Kristo Yesu, na mtume niliyeteuliwa na kuitwa kwa ajili ya kuhubiri Habari Njema ya Mungu.[#1:1-7 Kulingana na mtindo wa kuandika barua nyakati hizo, Paulo anajitambulisha kwa kutaja jina lake na kuwataja walengwa wa barua hii pamoja na salamu. Paulo alijulikana pia kwa jina lake lingine la Kiyahudi: Saulo (Mate 7:57—8:3; 9:1-30).; #1:1 Paulo anapojiita aghalabu anataka ieleweke kwamba yeye ana wajibu mpya na anayemtumikia ni mpya. Anawaondolea mashaka wale waliomfahamu kama mpinzani wa Yesu Kristo na muuaji wa Wakristo. Neno analitumia mara kwa mara katika barua zake (taz Gal 1:10; Tito 1:1; 2Tim 2:24); katika Kigiriki ni “doulos” ambalo lamaanisha pia mtumwa.; #1:1 Mtume ni mtu aliyetumwa na fulani afanye kazi fulani, apeleke ujumbe au afanye kwa mikono yake aliloagizwa afanye. Jina hilo lawataja hasa wale kumi na wawili ambao walikuwa na Yesu wakati alipokuwa hapa duniani (Luka 6:13). Neno hili lakini lilitumika pia kwa wanafunzi wengine wa Yesu Kristo (Mate 14:4,14; Rom 16:7; 1Kor 12:28; Efe 4:1). Paulo anajiona kuwa sawa na wale kumi na wawili (taz 1Kor 9:1-2) na ujumbe wake kuwa wenye mamlaka sawa na ujumbe wao.; #1:1 Tafsiri nyingine “Injili ya Mungu”. Yahusu ujumbe juu ya Yesu Kristo na pia juu ya ujumbe alioleta Yesu Kristo kuhusu ufalme wa Mungu.]
2Hapo kale, Mungu aliwaahidi watu hii Habari Njema kwa njia ya manabii wake katika Maandiko Matakatifu.
3Hii Habari Njema inamhusu Mwana wa Mungu, Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kuhusu ubinadamu wake, alikuwa mzawa wa Daudi;
4kuhusu utakatifu wake wa kimungu, alithibitishwa kwa uwezo mkuu kwamba ni Mwana wa Mungu kwa kufufuliwa kutoka kwa wafu.[#1:4 Kwa aya iliyotangulia (aya ya 3), Paulo anaanza kumbainisha Yesu Kristo katika hali mbili: kama mtu (neno kwa neno kama mzawa wa Daudi) na hivyo kukamilisha matazamio na matumaini ya Kiyahudi juu ya Masiha (rejea Mat 1:1; Luka 3:23-32). Na ya pili anambainisha kama mwenye hali ya kimungu ambayo ilidhihirika kwa ukamilifu zaidi katika kufufuka kwake. Kwa hiyo Paulo alitangaza waziwazi kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, jambo ambalo linatajwa pia mara nyingi katika Injili (Marko 15:31 na Yoh 1:49).]
5Kwa njia yake, mimi nimepewa neema ya kuwa mtume, ili kwa ajili yake niwaongoze watu wa mataifa yote wapate kuamini na kutii.[#1:5 Rejea Rom 16:26 ambapo barua hii inaishia kwa wazo hilo hilo. Taz pia Ebr 5:9; 1Pet 1:22.]
6Nyinyi ni miongoni mwa watu hao; mmeitwa muwe watu wake Yesu Kristo.
7Basi, nawaandikia nyinyi nyote mlioko Roma ambao Mungu anawapenda, akawateua muwe watu wake. Nawatakieni neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.[#1:7 Tafsiri nyingine: lakini maana halisi ni hali kamilifu isiyo na kosa ingawaje na hiyo inakidhi watu wa Mungu, ila yahusu watu walio wake Mungu mwenyewe, au waliotengwa kuwa mali yake. Kwa hiyo ni msemo ambao Paulo atautumia mara nyingi kutaja jumuiya ya kanisa ambayo ni ya watu walioitwa na Mungu (Rom 8:30) wakafanywa watakatifu.]
8Awali ya yote, namshukuru Mungu wangu kwa njia ya Yesu Kristo kwa ajili yenu nyote, kwa sababu imani yenu inasikika duniani kote.
9Mungu, ambaye ninamtumikia kwa moyo wangu wote katika kuhubiri Habari Njema ya Mwanae, ni shahidi wangu kwamba ninawakumbukeni[#1:9 Taz aya ya 1: “Habari Njema ya Mungu”.]
10daima katika sala zangu. Namwomba Mungu akipenda, anipatie nafasi nzuri ya kuja kwenu sasa.
11Kwa maana ninatamani sana kuwaoneni ili nipate kuwagawieni zawadi ya kiroho na kuwaimarisha.
12Ndiyo kusema, tutaimarishana: imani yenu itaniimarisha mimi, na yangu itawaimarisha nyinyi.
13Ndugu zangu, nataka mjue kwamba mara nyingi nilikusudia kuwatembeleeni, lakini mpaka sasa nimezuiwa. Ningependa kupata mafanikio mema kati yenu kama nilivyopata kati ya watu wa mataifa mengine.[#1:13 Hapa Paulo hataji hayo mafanikio anayotarajia, lakini kutokana na kazi aliyokwisha fanya kati ya watu wa mataifa mengine ni wazi kuwa alitumaini kuwa atapokelewa vizuri, na wengi washirikiane naye kwa kupenda kusikia mahubiri yake na kuimarishwa kiroho (taz aya ya 11 na ya 12. Ling aya ya 15).]
14Ninalo jukumu kwa watu wote, waliostaarabika na wasiostaarabika, wenye elimu na wasio na elimu.[#1:14 Neno kwa neno “Wagiriki na wasio Wagiriki”. Wagiriki kama vile Waroma walichukuliwa kuwa ni watu walioendela na wote wengine duniani kuwa watu wasio na maendeleo yoyote.]
15Ndiyo maana ninatamani pia kuihubiri Habari Njema kwenu nyinyi mlioko huko Roma.
16Sioni aibu kutangaza Habari Njema; yenyewe ni nguvu ya Mungu inayowaokoa wote wanaoamini: Wayahudi kwanza na wasio Wayahudi pia.[#1:16 Tamko hili ni muhimu sana katika barua zote za Paulo na hasa katika barua hii kwa Waroma. Hapa Paulo anataja kwa kifupi mada au wazo muhimu ambalo atalipanua kwa ukamilifu zaidi katika sehemu yote inayofuata ya barua hii (rejea hasa 3:21-4:25). Kwake Paulo kuamini kunajumuisha kitendo ambacho kwacho binadamu hukubali kwa moyo wake wote hatua ya wokovu ambayo Mungu kwa kupenda kwake alichukua, akaitekeleza kwa njia ya Yesu Kristo. Imani hiyo hujumuisha utii (aya 5), huonekana hasa katika taabu (2Thes 1:4) na hufanya kazi kwa njia ya mapendo (Gal 5:6). Paulo, mara nyingi hutofautisha imani hii na matendo au kazi za binadamu (rejea Rom 9:32) au na sheria (rejea Rom 3:28), ili kuonesha kwamba binadamu hawezi kufikia wokovu kwa mastahili yake mwenyewe ila kama zawadi ya Mungu kwa wote. Rejea Yoh 3:15-16; Rom 10:9-13.; #1:16 Mungu alikuwa amewapa Wayahudi ahadi zake kabla ya wengine (rejea Mate 13:46; Rom 3:1-2; 9:1—11:32).]
17Kwa maana Habari Njema inaonesha wazi jinsi Mungu anavyowakubali watu kuwa waadilifu; jambo hili hufanyika kwa imani, tangu mwanzo mpaka mwisho; kama ilivyoandikwa: “Mwadilifu kwa imani ataishi.”[#1:17 Ili kueleza kitendo au kazi ya Mungu ya wokovu Paulo anataja kitendo cha Mungu ambacho kwacho humfanya mwenye dhambi kuwa mwadilifu na kumwondoa kutoka nguvu za uovu akimweka katika uhusiano wa urafiki naye na kumwalika aishi uhai mpya (rejea hasa Rom 3:21-27; 5:1-2; 8:1-4). Hata hivyo ni katika hukumu ya mwisho tu ndipo Mungu atakapofanya tamko lake la kudumu kuhusu mtu kuwa mwadilifu na kuwa na uhai wa milele (Rom 2:5-11).; #1:17 Rom 3:28; Gal 2:16,20. Fungu la maneno “kwa imani tangu mwanzo mpaka mwisho” neno kwa neno ni “toka imani hata imani”.; #1:17 Maneno yanayokaririwa pia katika Gal 3:11; Ebr 10:38. Maneno hayo yanaweza pia kutafsiriwa kama: “Aliye mwadilifu, ataishi kwa imani.” Kwa kifupi, wokovu huwajia wale wanaomwamini Yesu kama Mwana wa Mungu na mwokozi wa ulimwengu.]
18Ghadhabu ya Mungu imedhihirishwa kutoka mbinguni dhidi ya uasi na uovu wote wa binadamu ambao kwa njia zao mbaya wanaupinga ukweli usijulikane.
19Kwa maana, yote yanayoweza kujulikana juu ya Mungu ni wazi kwao; maana Mungu mwenyewe ameyadhihirisha.
20Tangu Mungu alipoumba ulimwengu, uwezo wake wa milele na uungu wake, ingawa havionekani kwa macho, vinafahamika wazi. Watu wanaweza kuyajua mambo hayo kutokana na vitu hivyo alivyoumba Mungu. Kwa hiyo hawana njia yoyote ya kujitetea![#1:19-20 Paulo anataka kusema dhahiri kwamba watu wote wangepaswa kujua namna Mungu anavyowataka waishi kwa kuona jinsi alivyouumba ulimwengu.]
21Ingawa wanajua kuna Mungu, lakini hawampi heshima anayostahili, wala hawamshukuru. Badala yake, fikira zao zimekuwa batili na akili zao tupu zimejaa giza.[#1:21 Katika Biblia “giza” mara nyingi huwakilisha adhabu na kifo (Kumb 28:29; Zab 14:33; Isa 5:30. Taz pia Efe 4:17-18).]
22Wanajidai kuwa wenye hekima, kumbe ni wapumbavu.
23Wanaacha kumwabudu Mungu aishiye milele, na badala yake, wanaabudu sanamu zilizo mfano wa binadamu ambaye hufa, mfano wa wanyama, ndege, au wanyama watambaao.[#1:23 Ilikatazwa katika sheria ya Mose kuabudu kitu kingine badala ya Mungu mwenyewe (Kut 20:3-4). Wakati wa Paulo mataifa mengi kama Waroma na Wagiriki na watu wengine waliabudu sanamu za miungu au kuwajengea mahali pa kutambikia.]
24Kwa sababu hiyo, Mungu amewaacha wafuate tamaa mbaya za mioyo yao na kufanyiana mambo ya aibu kwa miili yao.
25Wanaubadili ukweli juu ya Mungu kwa uongo; wanaheshimu na kuabudu kiumbe badala ya Muumba mwenyewe, ambaye ndiye astahiliye sifa milele! Amina.[#1:25 Wazo hili laweza pia kutafsiriwa kama: “Badala ya kumfuata Mungu wa kweli, wamefuata miungu ya uongo”.]
26Kwa hiyo, Mungu amewaacha wafuate tamaa mbaya. Hata wanawake wanabadili matumizi yanayopatana na maumbile.
27Nao wanaume hali kadhalika, wanaacha kufuata matumizi ya maumbile ya mume na mke, wakawakiana tamaa wao kwa wao. Wanaume wanafanyiana mambo ya aibu, na hivyo wanajiletea wenyewe adhabu wanayostahili kwa vitendo vyao viovu.
28Kwa vile watu walikataa kumtambua Mungu, Mungu amewaacha katika fikira zao potovu, wakafanya yale ambayo hawangestahili kufanya.
29Wamejaa kila aina ya uovu, dhuluma, ulafi na ufisadi. Wamejaa wivu, uuaji, ugomvi, udanganyifu na nia mbaya; husengenya,
30na kusingiziana; ni watu wa kuchukiza kwa Mungu, wafidhuli, wenye kiburi na majivuno; hodari sana katika kutenda mabaya, na hawawatii wazazi wao;
31hawana dhamiri, hawatimizi ahadi zao, hawana wema wala huruma kwa wengine.
32Wanajua kwamba sheria ya Mungu yasema kwamba watu wanaoishi mithili hiyo, wanastahili kifo. Zaidi ya hayo, siyo tu kwamba wanafanya mambo hayo wao wenyewe, bali hata huwapongeza wale wanaofanya mambo hayohayo.