Walawi 22

Walawi 22

Matumizi ya sadaka takatifu

1Bwana akamwambia Musa,

2“Mwambie Haruni na wanawe kushughulikia kwa uangalifu sadaka takatifu Waisraeli wanazoziweka wakfu kwangu, ili wasilinajisi Jina langu takatifu. Mimi ndimi Bwana .

3“Waambie: ‘Katika vizazi vijavyo, ikiwa yeyote wa wazao wako ni najisi, naye akakaribia sadaka takatifu zile Waisraeli wanazoweka wakfu kwa Bwana , mtu huyo lazima akatiliwe mbali na uso wangu. Mimi ndimi Bwana .

4“ ‘Ikiwa mzao wa Haruni ana ugonjwa wa ngozi unaoambukiza au anatokwa na usaha mwilini, hawezi kula sadaka takatifu hadi atakasike. Pia atakuwa najisi akigusa kitu chochote kilicho najisi kutokana na kugusa maiti, au akigusa mtu aliyetokwa na shahawa,

5au akigusa kitu chochote kinachotambaa kimfanyacho mtu najisi, au mtu yeyote awezaye kumtia unajisi, hata unajisi uwe gani.

6Mtu anayegusa kitu chochote cha aina hiyo atakuwa najisi hadi jioni. Kamwe hatakula sadaka yoyote takatifu hadi yeye mwenyewe awe ameoga kwa maji.

7Jua linapotua, atakuwa safi, na baadaye anaweza kula sadaka takatifu, kwa kuwa ni vyakula vyake.

8Kamwe asile nyama ya mzoga wala iliyoraruliwa na wanyama pori, naye akatiwa unajisi kwa hilo. Mimi ndimi Bwana .

9“ ‘Makuhani lazima washike maagizo yangu ili wasiwe na hatia, wakafa kwa kuyadharau. Mimi ndimi Bwana ninayewafanya watakatifu.

10“ ‘Hakuna mtu yeyote asiye wa jamaa ya kuhani anayeruhusiwa kula sadaka takatifu, hata mgeni wa kuhani au mfanyakazi wake haruhusiwi kuila.

11Lakini ikiwa kuhani amenunua mtumwa kwa fedha, au mtumwa amezaliwa katika nyumba ya kuhani huyo, mtumwa huyo aweza kula chakula cha huyo kuhani.

12Ikiwa binti ya kuhani ameolewa na mtu asiye kuhani, binti huyo haruhusiwi kula chochote cha matoleo matakatifu.

13Lakini ikiwa binti ya kuhani amekuwa mjane au amepewa talaka, naye hana watoto, na akarudi kuishi na jamaa ya baba yake kama wakati wa usichana wake, binti huyo anaweza kula chakula cha baba yake. Hata hivyo, mtu asiyeruhusiwa hawezi kula chochote katika chakula hiki.

14“ ‘Ikiwa mtu yeyote amekula sadaka takatifu kwa makosa, lazima atoe malipo ya sadaka hiyo kwa kuhani na kuongeza sehemu ya tano ya thamani ya sadaka hiyo.

15Kamwe makuhani wasiinajisi sadaka takatifu ambayo Waisraeli wameitoa kwa Bwana

16kwa kuwaruhusu kuzila sadaka hizo takatifu, na hivyo kuwaletea hatia ya kudaiwa malipo. Mimi ndimi Bwana niwafanyaye watakatifu.’ ”

Dhabihu zisizokubalika

17Bwana akamwambia Musa,

18“Sema na Haruni na wanawe, na Waisraeli wote uwaambie: ‘Ikiwa mmoja wenu, aliye Mwisraeli au mgeni anayeishi katika nchi ya Israeli, atatoa matoleo kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa kwa moto kwa Bwana , iwe kutimiza nadhiri au kuwa sadaka ya hiari,

19lazima amtoe mnyama dume asiye na dosari, akiwa ngʼombe, mbuzi au kondoo, ili aweze kukubalika kwa niaba yako.

20Kamwe usitoe kitu chochote chenye dosari kwa sababu hakitakubaliwa kwa niaba yako.

21Mtu yeyote aletapo sadaka ya amani kwa Bwana kutoka kundi la ngʼombe au la mbuzi ili kutimiza nadhiri maalum au sadaka ya hiari, lazima sadaka hiyo isiwe na dosari au waa ili ikubalike.

22Kamwe usimtolee Bwana mnyama aliye kipofu, aliyejeruhiwa wala aliye kilema, au chochote kilicho na uvimbe, au chenye upele au vidonda vinavyotoka usaha. Kamwe chochote cha aina hii kisiwekwe juu ya madhabahu kuwa sadaka iliyotolewa kwa Bwana ya kuteketezwa kwa moto.

23Lakini unaweza ukamtoa ngʼombe au kondoo mwenye kilema au aliyedumaa kuwa sadaka ya hiari, lakini hii haitakubalika kuwa sadaka ya kutimiza nadhiri.

24Kamwe usimtolee Bwana mnyama ambaye mapumbu yake yamejeruhiwa, au kuhasiwa, au kuraruliwa au kukatwa. Kamwe usifanye hivi katika nchi yako mwenyewe,

25na kamwe usikubali wanyama wa aina hii kutoka mkono wa mgeni ili kuwatoa wanyama hao kuwa chakula kwa Mungu wako. Wanyama hao hawatakubaliwa kwa niaba yako, kwa sababu wana vilema, nao wana dosari.’ ”

26Bwana akamwambia Musa,

27“Ndama, mwana-kondoo au mwana-mbuzi anapozaliwa, atabaki na mama yake kwa siku saba. Kuanzia siku ya nane na kuendelea anaweza kukubaliwa kuwa sadaka iliyotolewa kwa Bwana kwa kuteketezwa kwa moto.

28Usimchinje ngʼombe na ndama wake, au kondoo na kitoto chake siku moja.

29“Unapomtolea Bwana dhabihu ya shukrani, itoe kwa namna ambayo itakubalika kwa niaba yako.

30Ni lazima iliwe siku hiyo hiyo, pasipo kubakiza chochote hadi asubuhi. Mimi ndimi Bwana .

31“Shikeni maagizo yangu na kuyafuata. Mimi ndimi Bwana .

32Msilinajisi Jina langu takatifu. Lazima nikubalike kuwa mtakatifu kwa Waisraeli. Mimi ndimi Bwana ninayewafanya watakatifu,

33na niliyewatoa katika nchi ya Misri niwe Mungu wenu. Mimi ndimi Bwana .”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.