Mika 1

Mika 1

1Neno la Bwana lilimjia Mika Mmoreshethi wakati wa utawala wa Yothamu, Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda, ufunuo aliouona kuhusu Samaria na Yerusalemu.

2Sikieni, enyi mataifa, enyi nyote,

sikilizeni, ee dunia na wote mliomo,

ili Bwana Mwenyezi ashuhudie dhidi yenu,

Bwana kutoka Hekalu lake takatifu.

Hukumu dhidi ya Samaria na Yerusalemu

3Tazama! Bwana anakuja kutoka mahali pake;

anashuka na kukanyaga

mahali palipoinuka juu pa dunia.

4Milima inayeyuka chini yake

na mabonde yanagawanyika

kama nta mbele ya moto,

kama maji yanayotiririka kasi

kwenye mteremko.

5Yote haya ni kwa sababu ya kosa la Yakobo,

ni kwa sababu ya dhambi za nyumba ya Israeli.

Kosa la Yakobo ni lipi?

Je, sio Samaria?

Je, mahali pa juu pa Yuda pa kuabudia ni nini?

Je, sio Yerusalemu?

6“Kwa hiyo nitaufanya Samaria kuwa lundo la kokoto,

mahali pa kuotesha mizabibu.

Nitayamwaga mawe yake katika bonde

na kuacha wazi misingi yake.

7Sanamu zake zote

zitavunjwa vipande vipande;

zawadi zake zote za Hekalu

zitachomwa kwa moto;

nitaharibu vinyago vyake vyote.

Kwa kuwa alikusanya zawadi zake

kutokana na ujira wa kahaba,

nazo zitatumika tena

kulipa mishahara ya kahaba.”

Kulia na kuomboleza

8Kwa ajili ya hili nitalia na kuomboleza;

nitatembea bila viatu na tena uchi.

Nitabweka kama mbweha

na kuomboleza kama bundi.

9Kwa sababu jeraha lake halitibiki;

limekuja kwa Yuda.

Limefika hasa kwenye lango la watu wangu,

hata Yerusalemu kwenyewe.

10Usiliseme hili huko Gathi;

usilie hata kidogo.

Huko Beth-le-Afra

gaagaa mavumbini.

11Piteni mkiwa uchi na wenye aibu,

ninyi mnaoishi Shafiri.

Wale wanaoishi Saanani

hawatatoka nje.

Beth-Eseli iko katika maombolezo;

kinga yake imeondolewa kwako.

12Wale wanaoishi Marothi wanagaagaa kwa maumivu

wakingoja msaada,

kwa sababu maangamizi yamekuja

kutoka kwa Bwana ,

hata katika lango la Yerusalemu.

13Enyi mnaoishi Lakishi,

fungeni farasi kwenye magari ya vita.

Mlikuwa chanzo cha dhambi

kwa Binti Sayuni,

kwa kuwa makosa ya Israeli

yalikutwa kwako.

14Kwa hiyo utaipa Moresheth-Gathi

zawadi za kuagana.

Mji wa Akzibu utaonesha wazi udanganyifu

kwa wafalme wa Israeli.

15Nitawaleteeni atakayewashinda

ninyi mnaoishi Maresha.

Yeye aliye utukufu wa Israeli

atakuja Adulamu.

16Nyoeni nywele zenu katika kuomboleza

kwa ajili ya watoto wenu mnaowafurahia;

jifanyieni upara kama tai,

kwa kuwa watawaacha

na kwenda uhamishoni.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.