Zaburi 48

Zaburi 48

Zaburi 48

Sayuni, mji wa Mungu

1Bwana ni mkuu, anayestahili kusifiwa sana,

katika mji wa Mungu wetu,

mlima wake mtakatifu.

2Ni mzuri katika kuinuka juu kwake,

furaha ya dunia yote.

Kama vilele vya juu vya Safoni ni Mlima Sayuni,

mji wa Mfalme Mkuu.

3Mungu yuko katika ngome zake;

amejionesha mwenyewe kuwa ngome yake.

4Wafalme walipounganisha nguvu,

waliposonga mbele pamoja,

5walimwona, wakashangaa,

wakakimbia kwa hofu.

6Kutetemeka kuliwashika huko,

maumivu kama ya mwanamke

mwenye uchungu wa kuzaa.

7Uliwaangamiza kama meli za Tarshishi

zilizovunjwa na upepo wa mashariki.

8Kama tulivyokuwa tumesikia,

ndivyo tulivyoona

katika mji wa Bwana wa majeshi,

katika mji wa Mungu wetu:

Mungu ataufanya uwe salama milele.

9Ee Mungu, hekaluni mwako

tunatafakari upendo wako usiokoma.

10Ee Mungu, kama jina lako lilivyo,

sifa zako zinafika hadi miisho ya dunia,

mkono wako wa kuume umejazwa na haki.

11Mlima Sayuni unashangilia,

vijiji vya Yuda vinafurahi

kwa sababu ya hukumu zako.

12Tembeeni katika Sayuni,

uzungukeni mji,

hesabuni minara yake;

13yatafakarini vyema maboma yake,

angalieni ngome zake,

ili mpate kusimulia habari zake

kwa kizazi kijacho.

14Kwa kuwa huyu Mungu ni Mungu wetu milele na milele;

atakuwa kiongozi wetu hata mwisho.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.