The chat will start when you send the first message.
1Mwenye kugusa lami atatiwa uchafu; naye mwenye kufuatana na mwenye kiburi atapata kufanana naye.
2Usijitwike mzigo upitao nguvu zako; wala usishirikiane na mtu aliye tajiri kuliko wewe. Jinsi gani chungu kushirikiana na birika? Hiyo itagonga na hicho kitavunjwa.
3Tajiri hudhulumu, akaogofya; maskini hudhulumiwa, akasihi.
4Iwapo una faida kwake, tajiri atachuma kwako; ukihitaji atakuacha.
5Kama una kitu, atakaa nawe; hata utakapofilisika, hajuti.
6Je! Ana haja nawe? Basi atakudanganya, na kukushawishi, na kukutia tumaini; atakupa maneno mazuri na kusema, Unahitaji nini?
7Naye atakutahayarisha kwa karamu zake; hata amekukumbia yote mara mbili tatu. Mwishowe atakufanyizia mzaha; atakuahirisha, na kukuacha, na kutikisa kichwa chake.
8Ujihadhari usije ukadanganyika na kufedheheshwa katika uchangamfu wako.
9Mkuu akikualika na uwe makini, hivyo atazidi kukualika.
10Usijitangulize kwake, usije ukakatazwa; wala usijitenge naye, usije ukasahauliwa.
11Usifanye kusema naye kama na mwenzako; wala usisadiki maneno yake mengi; yaani, kwa maongezi mengi atakujaribu, na kwa kukunjua uso atakupeleleza.
12Mtu asiyeficha moyoni mwake yaliyosemwa hana rehema; maana hatajizuia na kuhizi wala na kufunga;
13basi ujihadhari uwe macho, maadamu unakwenda katikati ya hatari ya kuanguka.
14-15Kila kiumbe hupenda kilichofanana nacho, na kila mwanadamu humpenda aliyefanana naye.
16Wanyama wote huandamana aina kwa aina; vile vile mwanadamu ataambatana na mmojawapo wa aina yake.
17Jinsi gani mbwamwitu ashirikiane na mwana-kondoo? Vivyo hivyo mwenye dhambi na mwenye haki.
18Kuna amani gani kati ya fisi na mbwa? Tena amani gani kati ya tajiri na maskini?
19Punda mwitu ni mawindo ya simba nyikani; ndivyo maskini walivyo malisho ya tajiri.
20Unyonge ni chukizo kwa mwenye kiburi; na umaskini ni chukizo kwa tajiri.
21Tena tajiri akitikisika huegemezwa na rafiki zake; mnyonge akiisha kuanguka husukumizwa mbali na rafiki zake.
22Tajiri akianguka, wapo wasidizi wengi; hata akinena yasiyoneneka, watu humkiri kuwa ana haki; mnyonge huanguka, na watu humshutumu; hata akitoa maneno ya hekima hakuna ampishaye.
23Tajiri anena, na wote wanyamaza na yale ayanenayo huyasifu hata mawinguni; maskini anena, nao husema, Nani huyu? Na iwapo amejikwaa, kumbe! Watazidi kumwangusha.
24Lakini utajiri pasipo dhambi ni mwema; na umaskini ni mbaya ukitoka katika ubaya.
25Moyo wa mtu hufanya kubadili uso,
Kwamba ni kwa wema au kwa ubaya.
26Uso mkunjufu hufunua moyo ulio fani;
Na kubuni mifano ni kuchosha akili.