Danieli 5

Danieli 5

Karamu ya Belshaza

1Mfalme Belshaza, aliwafanyia wakuu wake elfu karamu kubwa akanywa divai mbele ya hao elfu.[#Est 1:3; Isa 21:5; Yer 51:39,57; Nah 1:10; Mk 6:21]

2Belshaza, alipokuwa akionja ile divai, akaamuru wavilete vile vyombo vya dhahabu na fedha, ambavyo baba yake, Nebukadneza, alivitoa katika hekalu lililokuwako Yerusalemu; ili kwamba mfalme, na wakuu wake, na wake zake, na masuria wake, wapate kuvinywea.[#Mit 20:1]

3Basi wakavileta vile vyombo vya dhahabu, vilivyotolewa katika hekalu la nyumba ya Mungu lililokuwako Yerusalemu; na mfalme na wakuu wake, na wake zake, na masuria wake, wakavinywea.

4Wakanywa divai, wakaisifu miungu ya dhahabu, na ya fedha, na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe.[#Zab 115:4-8; Ufu 9:20]

Maandiko ukutani

5Saa iyo hiyo vikatokea vidole vya mkono wa mwanadamu, vikaandika katika chokaa ya ukuta wa nyumba ya enzi ya mfalme, mahali palipokielekea kinara; naye mfalme akakiona kiganja cha ule mkono ulioandika.[#Dan 4:31]

6Ndipo uso wa mfalme ukambadilika; fikira zake zikamfadhaisha; viungo vya viuno vyake vikalegea; magoti yake yakagongana.[#Ayu 18:11; Nah 2:10]

7Mfalme akalia kwa sauti kubwa, akaamuru waletwe wachawi, na Wakaldayo na wanajimu. Mfalme akanena, akawaambia wenye hekima wa Babeli, mtu awaye yote atakayesoma maandiko haya, na kunionesha tafsiri yake, atavikwa mavazi ya rangi ya zambarau, na kuwa na mkufu wa dhahabu shingoni mwake, naye atakuwa mtu wa tatu katika ufalme.[#Isa 47:13; Dan 6:2]

8Basi wakaingia wenye hekima wote wa mfalme; lakini hawakuweza kuyasoma yale maandiko, wala kumjulisha mfalme tafsiri yake.[#Mwa 41:8]

9Ndipo mfalme Belshaza akahangaika sana, uso wake ukambadilika, na wakuu wake wakaona fadhaa.

10Basi malkia, kwa sababu ya maneno ya mfalme na ya wakuu wake, akaingia katika nyumba ya karamu; malkia akanena, akasema, Ee mfalme, uishi milele; fikira zako zisikufadhaishe; wala uso wako usibadilike.[#Dan 3:9]

11Yuko mtu katika ufalme wako, ambaye roho ya miungu watakatifu inakaa ndani yake; na katika siku za baba yako nuru na ufahamu na hekima zilionekana ndani yake; na mfalme Nebukadneza, baba yako, naam, mfalme, baba yako, akamfanya kuwa mkuu wa waganga, na wachawi, na Wakaldayo, na wanajimu;[#Dan 4:9]

12kwa kuwa roho njema kupita kiasi, na maarifa, na ufahamu, na uwezo wa kufasiri ndoto, na kufunua maneno ya fumbo, na kufungua mafundo, zilionekana katika Danieli huyo, ambaye mfalme alimwita Belteshaza. Basi na aitwe Danieli, naye ataionesha tafsiri.[#Dan 6:3]

13Ndipo Danieli akaletwa mbele ya mfalme. Na Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Je! Wewe ndiwe Danieli yule, aliye mmoja wa wana wa Yuda waliohamishwa, ambao mfalme, baba yangu, aliwaleta huku toka Yerusalemu?

14Nimesikia habari zako, kwamba roho ya miungu imo ndani yako, na kwamba nuru na ufahamu na akili bora zimeonekana kwako.

15Basi sasa, watu wenye hekima na wachawi wameletwa mbele yangu, wapate kulisoma andiko hili, na kunijulisha tafsiri yake; lakini hawakuweza kunijulisha tafsiri ya jambo hili.

16Lakini nimesikia habari zako, kwamba waweza kuleta tafsiri, na kufumbua mafumbo; haya! Kama ukiweza kulisoma andiko hili, na kunijulisha tafsiri yake, utavikwa mavazi ya rangi ya zambarau, na kuwa na mkufu wa dhahabu shingoni mwako, nawe utakuwa mtu wa tatu katika ufalme.

Danieli afasiri ndoto ya pili

17Ndipo Danieli akajibu, akasema mbele ya mfalme; Zawadi zako baki nazo wewe mwenyewe; na thawabu zako mpe mtu mwingine; lakini nitamsomea mfalme maandiko haya, na kumjulisha tafsiri yake.

18Kwa habari zako, Ee mfalme, Mungu Aliye Juu alimpa Nebukadneza, baba yako, ufalme, na ukuu, na fahari, na utukufu;[#Dan 2:37]

19na kwa sababu ya ule ukuu aliompa, watu wa kabila zote, na mataifa, na lugha, wakatetemeka na kuogopa mbele yake; aliyetaka kumwua alimwua; na aliyetaka kumwacha hai, alimwacha hai; aliyetaka kumtukuza, alimtukuza; na aliyetaka kumshusha, alimshusha.[#Yer 25:9; Dan 3:4]

20Lakini moyo wake ulipoinuliwa, na roho yake ilipokuwa ngumu akatenda kwa kiburi, alishushwa katika kiti chake cha enzi, nao wakamwondolea utukufu wake.[#Kut 9:17; Mit 16:5; Isa 14:12-17; Dan 4:30]

21Akafukuzwa mbali na wanadamu, moyo wake ukafanywa kuwa kama moyo wa mnyama, na makao yake yalikuwa pamoja na punda mwitu; akalishwa majani kama ng'ombe, mwili wake ukalowa maji kwa umande wa mbinguni; hata alipojua ya kuwa Mungu Aliye Juu ndiye anayetawala katika ufalme wa wanadamu, na ya kuwa humweka juu yake yeye amtakaye, awaye yote.[#Dan 4:17,32; Kut 9:14-16]

22Na wewe, mwanawe, Ee Belshaza, hukujinyenyekeza moyo wako, ijapokuwa ulijua hayo yote.[#2 Nya 33:23; Zab 119:46]

23Bali umejiinua juu ya Bwana wa mbingu; nao wamevileta vyombo vya nyumba yake mbele yako; na wewe, na wakuu wako, na wake zako, na masuria wako, mmevinywea; nawe umeisifu miungu ya fedha na ya dhahabu na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe; wasioona, wala kusikia, wala kujua neno lolote; na Mungu yule, ambaye pumzi yako i mkononi mwake, na njia zako zote ni zake, hukumtukuza.[#Isa 37:23; 46:6,7; Yer 50:20; Ufu 13:6; Zab 115:5; 139:3; Hab 2:18; Ayu 31:4; Mit 20:24]

24Ndipo kile kiganja cha ule mkono kikaletwa kutoka mbele zake, na maandiko haya yameandikwa.

25Na maandiko yaliyoandikwa ni haya; MENE, MENE, TEKELI, NA PERESI.

26Na tafsiri ya maneno haya ni hii; MENE, Mungu ameuhesabu ufalme wako na kuukomesha.[#Yer 25:12]

27TEKELI, umepimwa katika mizani nawe umeonekana kuwa umepunguka.[#Zab 62:9; Yer 6:30]

28PERESI, ufalme wako umegawanyika, nao wamepewa Wamedi na Waajemi.[#Isa 21:2; Ezr 1:1; Dan 9:1; 6:28]

29Ndipo Belshaza akatoa amri, nao wakamvika Danieli mavazi ya rangi ya zambarau, wakatia mkufu wa dhahabu shingoni mwake, wakapiga mbiu kutangaza habari zake, ya kwamba yeye ni mtu wa tatu katika ufalme.

30Usiku huo huo Belshaza, mfalme wa Wakaldayo, akauawa.[#Yer 51:31,39,57]

31Na Dario, Mmedi, akaupokea ufalme, naye umri wake alikuwa na miaka sitini na miwili.[#Dan 9:1]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya