Kumbukumbu la Torati 21

Kumbukumbu la Torati 21

Sheria kuhusu uuaji wa watu wasiojulikana

1Aonekanapo mtu ameuawa katika nchi akupayo BWANA, Mungu wako, kuimiliki, amelala kondeni, wala haijulikani ni nani aliyempiga;[#Zab 9:12; Mit 28:17]

2na watoke nje wazee wako na waamuzi wako, nao wapime hapo mpaka miji iliyomzunguka huyo aliyeuawa;

3na iwe, mji ulio karibu na yule aliyeuawa, wale wazee wake mji huo watwae mtamba katika kundi la ng'ombe, ambaye hajafanya kazi, wala hajakokota jembe la nira;

4wazee wa mji huo na wamshushe yule mtamba mpaka bonde lenye maji ya mtoni, lisilolimwa wala kupandwa, wakamvunje yule mtamba shingo yake humo bondeni;

5nao makuhani wana wa Lawi wasongee karibu, kwa kuwa ndio aliowachagua BWANA, Mungu wako, wamtumikie, na kubariki katika jina la BWANA na kila neno lishindaniwalo, na kila pigo, litakuwa kwa kufuata maneno yao;[#1 Nya 23:13; Kum 17:8,9]

6na wazee wote wa mji ule, ulio karibu sana na yule aliyeuawa, na waoshe mikono yao juu ya huyo mtamba aliyevunjwa shingo yake humo bondeni;[#Ayu 9:30; Zab 19:12; 73:13; Yer 2:22; Mt 27:24; Ebr 9:10]

7na wajibizane kwamba, Mikono yetu haikumwaga damu hii, wala macho yetu hayakuiona.[#2 Sam 3:28]

8Ee BWANA, wasamehe watu wako Israeli, uliowakomboa, wala usiiache damu ya asiye makosa ikakaa katikati ya watu wako Israeli. Na ile damu utasamehewa kwao.[#Yer 26:15; Eze 22:3; Yon 1:14; 1 The 2:15,16]

9Ndivyo utakavyoindoa damu ya asiye makosa katikati yako, utakapofanya yaliyo sawa machoni pa BWANA.[#Kum 19:13]

Mateka wa kike

10Utakapokwenda vitani kupigana juu ya adui zako, na BWANA, Mungu wako, awatiapo mikononi mwako, nawe uwachukuapo mateka,[#2 Nya 32:8; Yos 21:44]

11ukaona kati ya mateka mwanamke mzuri, ukafanya tamaa kwake, ukawaza kumtwaa kuwa mkeo;

12ndipo umchukue kwenu nyumbani kwako, naye atanyoa kichwa, akate na kucha;

13avue na mavazi ya uteka wake akae nyumbani mwako, awakalie matanga babaye na mamaye mwezi mzima, kisha uingie kwake uwe mumewe, naye awe mkeo.[#Zab 45:10]

14Tena utakapokuwa huna furaha naye, mpe ruhusa aende atakako; lakini usimwuze kabisa kwa fedha, usimfanye kama mtumwa, kwa kuwa ulimtweza.[#Mwa 34:2; Amu 19:24]

Haki ya mzaliwa wa kwanza

15Ikiwa mtu ana wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa;[#Mwa 29:33]

16ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu;[#2 Nya 11:19; 21:3; Rum 8:29]

17lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye.[#Mwa 25:5,6,31; 1 Nya 5:1; Mwa 49:3]

Watoto wasiotii

18Mtu akiwa na mwana mkaidi, mshupavu, asiyetii sauti ya baba yake, wala sauti ya mama yake, nao wajapomwadhibu hawasikizi,[#Kut 20:12; 21:15,17; Law 19:3; 21:9; Mit 1:8; 15:5; Efe 6:1]

19ndipo babaye na mamaye na wamkamate, na kumpeleka kwa wazee wa mji wake, katika lango la mahali pake;

20wawaambie wazee wa mji wake, Huyu mwana wetu ni mkaidi, mshupavu, hasikizi sauti yetu; ni mwasherati, tena ni mlevi.

21Wanaume wote wa mji wake na wamtupie mawe, afe; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako; na Israeli wote watasikia na kuogopa.[#Kum 19:19; 13:11]

Sheria nyinginezo

22Ikiwa mtu ametenda dhambi ipasayo kufa, akauawa, nawe ukamtundika juu ya mti;[#Kum 22:26; 1 Sam 26:16; Mt 26:66; Mdo 23:29]

23mzoga wake usikae usiku kucha juu ya mti; lazima utamzika siku iyo hiyo; kwani aliyetundikwa amelaaniwa na Mungu; usije ukatia unajisi katika nchi yako akupayo BWANA, Mungu wako, iwe urithi wako.[#Gal 3:13; Yos 8:29; Yn 19:31; Law 18:25; Hes 35:34]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya