Yeremia 28

Yeremia 28

Hanania ampinga Yeremia na kufa

1Ikawa, katika mwaka ule ule, mwanzo wa kutawala kwake Sedekia, mfalme wa Yuda, mwaka wa nne, mwezi wa tano, Hanania, mwana wa Azuri, nabii, wa Gibeoni, akasema nami ndani ya nyumba ya BWANA, mbele ya makuhani na watu wote, akisema,[#Yer 27:1; 36:12; 2 Tim 2:8; 2 Pet 2:1; 2 Fal 24:18-20; 2 Nya 36:11-13]

2BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nimeivunja nira ya mfalme wa Babeli.[#Yer 27:12]

3Kabla haujatimia muda wa miaka miwili mizima, nitavirudisha mahali hapa vyombo vyote vya nyumba ya BWANA, ambavyo Nebukadneza, mfalme wa Babeli, aliviondoa kutoka mahali hapa, akavipeleka mpaka Babeli.[#2 Fal 24:13; 2 Nya 36:10; Yer 27:16-22]

4Nami nitamrudisha hapa Yekonia, mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, pamoja na mateka wote wa Yuda, waliokwenda Babeli, asema BWANA; maana nitaivunja nira ya mfalme wa Babeli.

5Ndipo nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, mbele ya makuhani, na mbele ya watu wote waliosimama ndani ya nyumba ya BWANA,

6naam, nabii Yeremia akasema, Amina, BWANA na atende hivi; BWANA ayatimize maneno yako uliyotabiri, kuvirudisha hapa vyombo vya nyumba ya BWANA na watu wote waliofungwa, toka Babeli, hadi mahali hapa.[#1 Fal 1:36; 1 Nya 16:36; Zab 41:13; 72:19; 89:52; Mit 6:13; 1 Kor 14:16; 2 Kor 1:20; Ufu 1:18]

7Lakini lisikilize sasa neno hili nilisemalo, masikioni mwako, na masikioni mwa watu wote,[#Kum 32:35; 1 Sam 2:9; Ayu 21:30; Mit 11:21; Zab 9:16; 34:21; Nah 1:2,3; Rum 2:2,3; Ebr 9:27; 12:29]

8Manabii walionitangulia, na waliokutangulia, walitabiri habari za vita, na za mabaya na za tauni juu ya nchi nyingi, na juu ya falme kubwa.

9Nabii atabiriye habari za amani, neno la nabii yule litakapotokea, ndipo nabii yule atakapojulikana, kweli kuwa BWANA amemtuma.[#Kum 18:22; Isa 8:20]

10Ndipo nabii Hanania akaitwaa hiyo nira iliyokuwa juu ya shingo ya Yeremia, akaivunja.[#1 Fal 22:24; Zab 10:13]

11Naye Hanania akanena mbele ya watu wote, akisema, BWANA asema hivi, Hivyo ndivyo nitakavyoivunja nira ya Nebukadneza, mfalme wa Babeli, kabla haujatimia muda wa miaka miwili kamili, na kuiondoa shingoni mwa mataifa yote. Basi nabii Yeremia akaenda zake.[#Yer 27:7; Mit 26:4]

12Ndipo neno la BWANA likamjia Yeremia, baada ya Hanania, nabii, kuivunja ile nira iliyokuwa juu ya shingo ya Yeremia, kusema,

13Nenda ukamwambie Hanania, ukisema, BWANA asema hivi, Umezivunja nira za mti; lakini badala yake utafanya nira za chuma.

14Maana BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nimetia nira ya chuma juu ya shingo ya mataifa haya yote, ili wamtumikie Nebukadneza, mfalme wa Babeli nao watamtumikia; nami nimempa wanyama wa nchi pia.[#Kum 28:48; Yer 27:4-7]

15Kisha nabii Yeremia akamwambia nabii Hanania, Sikia sasa, Ee Hanania; BWANA hakukutuma; lakini unawapa tumaini watu hawa kwa maneno ya uongo.[#Yer 20:6; 29:31]

16Basi BWANA asema hivi, Tazama, nakutuma uende zako toka juu ya uso wa nchi; mwaka huu utakufa, kwa sababu umenena maneno ya uasi juu ya BWANA.

17Basi nabii Hanania akafa, mwaka uo huo, mwezi wa saba.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya