The chat will start when you send the first message.
1Neno hili ndilo lililomjia Yeremia, kutoka kwa BWANA, katika siku za Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, kusema,[#2 Fal 23:36—24:6; 2 Nya 36:5-7; Yer 22:18; Dan 1:1]
2Nenda nyumbani kwa Warekabi, ukanene nao, ukawalete nyumbani kwa BWANA, katika chumba kimoja, ukawape divai wanywe.[#2 Fal 10:15; 1 Nya 2:55; 1 Fal 6:5]
3Basi nikamtwaa Yaazania, mwana wa Yeremia, mwana wa Habasinia, na ndugu zake, na wanawe wote, na nyumba yote ya Warekabi;
4nikawaleta ndani ya nyumba ya BWANA, ndani ya chumba cha wana wa Hanani, mwana wa Igdalia, mtu wa Mungu, kilichokuwa karibu na chumba cha wakuu, nacho kilikuwa juu ya chumba cha Maaseya, mwana wa Shalumu, bawabu;[#2 Fal 12:9; 1 Nya 9:18,19]
5nikaweka mabakuli yaliyojaa divai, na vikombe, mbele ya wana wa nyumba ya Warekabi, nikawaambia, Nyweni divai.
6Lakini wakasema, Hatutakunywa divai; kwa maana Yonadabu, mwana wa Rekabu, baba yetu, alituamuru, akisema, Msinywe divai, ninyi wala wana wenu, hata milele;[#Yer 35:2]
7wala msijenge nyumba, wala msipande mbegu, wala msipande mizabibu, wala msiwe nayo; bali siku zenu zote mtakaa katika hema; mpate kuishi siku nyingi katika nchi ambayo mtakaa ndani yake kama wageni.[#Kut 20:12; Kum 4:40; Mit 3:16; Efe 6:2,3]
8Nasi tumeitii sauti ya Yonadabu, mwana wa Rekabu, baba yetu, katika yote aliyotuamuru, kwamba tusinywe divai siku zetu zote, sisi, na wake zetu, na wana wetu, na binti zetu;[#Mit 1:8; Kol 3:20]
9wala tusijijengee nyumba za kukaa; wala hatuna shamba la mizabibu, wala shamba, wala mbegu;
10bali tumekaa katika hema, nasi tumetii; tukafanya sawasawa na yote aliyotuamuru Yonadabu, baba yetu.
11Lakini ikawa, Nebukadneza, mfalme wa Babeli, alipopanda akaingia nchi hii, ndipo tukasema, Haya! Twende Yerusalemu, kwa kuliogopa jeshi la Wakaldayo, na kwa kuliogopa jeshi la Washami; ndiyo maana sasa tunaishi Yerusalemu.[#2 Fal 24:1]
12Ndipo neno la BWANA likamjia Yeremia, kusema,
13BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Nenda ukawaambie wana wa Yuda, na wenyeji wa Yerusalemu, Je! Hamtaki kupokea mafundisho, myasikilize maneno yangu? Asema BWANA.[#Yer 32:33]
14Maneno ya Yonadabu, mwana wa Rekabu, aliyowaamuru wanawe, kwamba wasinywe divai, yametimizwa, na hata leo hawanywi; maana wanaitii hiyo amri ya baba yao; lakini mimi nimesema nanyi, nikiamka mapema na kunena, bali ninyi hamkunisikiliza mimi.[#2 Nya 36:15; Yer 7:13]
15Pia niliwatuma watumishi wangu wote, manabii, kwenu ninyi, nikiwatuma pasipo kukoma, nikisema, Rudini sasa, kila mtu na aiache njia yake mbaya, mkatengeneze matendo yenu, wala msiifuate miungu mingine, ili kuitumikia, nanyi mtakaa katika nchi hii, niliyowapa ninyi na baba zenu; lakini hamkutega masikio yenu, wala hamkunisikiliza.[#Yer 7:25; 3:14; 18:11; 25:5,6; Isa 1:16-19; 30:9; Hos 14:1-4; Mdo 26:20]
16Basi, kwa kuwa wana wa Yonadabu, mwana wa Rekabu, wameitimiza amri ya baba yao aliyowaamuru, lakini watu hawa hawakunisikiliza mimi;
17kwa sababu hiyo, asema BWANA, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli; Tazama nitaleta juu ya Yuda, na juu ya wenyeji wote wa Yerusalemu, mabaya yote niliyoyatamka juu yao; kwa sababu nimesema nao, wasinisikilize; nimewaita, wala hawakuniitikia.[#Law 26:14; Yos 23:15; Yer 15:3,4; 7:13; Mik 3:12; Mit 1:24; Isa 65:12]
18Naye Yeremia akawaambia watu wa nyumba ya Warekabi, BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa sababu mmeitii amri ya Yonadabu, baba yenu, na kuyashika maagizo yake yote, na kutenda sawasawa na yote aliyowaamuru;[#Kut 20:12]
19basi, kwa sababu hiyo, BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Yonadabu, mwana wa Rekabu, hatakosa kuwa na mzawa wa kusimama mbele zangu hata milele.[#Yer 15:19]