Mithali 17

Mithali 17

1Afadhali mego kavu pamoja na utulivu,

Kuliko nyumba yenye karamu nyingi pamoja na magomvi.

2Mtumwa atendaye kwa busara atamtawala mwana atendaye mambo ya aibu;

Tena atapata sehemu ya urithi kati ya ndugu.

3Kalibu ni kwa fedha, na tanuri kwa dhahabu;[#Zab 26:2; Mit 27:21; Yer 17:10; Mal 3:3]

Bali BWANA huijaribu mioyo.

4Mtenda mabaya husikiliza midomo ya uovu;

Na mwongo hutega sikio lake kusikiliza ulimi wa madhara.

5Amchekaye maskini humtukana Muumba wake;[#Ayu 31:29; Mit 24:17; Oba 1:12]

Naye aufurahiaye msiba hatakosa adhabu.

6Wana wa wana ndio taji la wazee,

Na utukufu wa watoto ni baba zao.

7Maneno mazuri hayapendezi kinywani mwa mpumbavu;

Sembuse midomo ya uongo kinywani mwa mkuu.

8Kipawa ni kama kito cha thamani machoni pake yeye aliye nacho;[#Mwa 39:21; Dan 6:3]

Kila kigeukapo hufanikiwa.

9Afunikaye kosa hutafuta kupendwa;

Bali yeye afichuaye siri hutenga rafiki.

10Lawama hupenya moyoni mwa mwenye ufahamu,

Kuliko mapigo mia moyoni mwa mpumbavu.

11Mtu mwovu hataki neno ila kuasi tu;

Kwa hiyo mjumbe mkali atatumwa kwake.

12Afadhali mtu akutwe na dubu jike aliyenyang'anywa watoto wake,

Kuliko na mpumbavu katika upumbavu wake.

13Yeye arudishaye mabaya badala ya mema,[#Yer 18:20; Rum 12:17; 1 The 5:15]

Mabaya hayataondoka nyumbani mwake.

14Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji;[#Mit 20:3; Mdo 6:1; Rum 12:18; 1 The 4:11]

Basi acheni ugomvi kabla haujafurika.

15Yeye asemaye kwamba asiye haki ana haki;[#Kut 23:7; Isa 5:23]

naye asemaye kwamba mwenye haki hana haki;

Hao wote wawili ni chukizo kwa BWANA.

16Nini maana yake, mpumbavu kuwa na fedha mkononi mwake ya kununulia hekima,

Ikiwa hana moyo wa ufahamu?

17Rafiki hupenda sikuzote;

Na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.

18Asiye na hekima hupeana mkono na mtu;

Na kuwa mdhamini wa mtu mwingine.

19Apendaye ugomvi hupenda dhambi;

Auinuaye sana mlango wake hutafuta uharibifu.

20Mtu mwenye moyo wa ukaidi hatapata mema;

Na mwenye ulimi wa upotovu huanguka katika misiba.

21Azaaye mpumbavu ni kwa huzuni yake mwenyewe;

Wala baba wa mpumbavu hana furaha.

22Moyo uliochangamka ni dawa nzuri;

Bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.

23Asiye haki hutoa rushwa kifuani,[#Kut 23:8]

Ili kuzipotosha njia za hukumu.

24Hekima huwa machoni pake mwenye ufahamu;[#Mhu 2:14]

Bali macho ya mpumbavu huwa katika ncha za dunia.

25Mwana mpumbavu ni huzuni kwa babaye,

Na uchungu kwa mamaye aliyemzaa.

26Tena kumwadhibu mwenye haki si vizuri;

Wala si vyema kuwapiga wakuu kwa unyofu wao.

27Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa;[#Yak 1:19]

Na mwenye roho ya utulivu ana busara.

28Hata mpumbavu akinyamaza, huhesabiwa hekima;

Akifumba midomo yake, huhesabiwa ufahamu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya