Mithali 23

Mithali 23

1Utakapoketi kwa chakula pamoja na mtawala,

Mwangalie sana yeye aliye mbele yako.

2Tena ujitie kisu kooni,

Kama ukiwa mlafi.

3Usivitamani vyakula vyake vya anasa;

Kwa maana ni vyakula vya hila.

4Usijitaabishe ili kupata utajiri;[#Mit 28:20; 3:5; Yn 6:27; 1 Tim 6:9; Rum 12:16]

Acha kuzitegemea akili zako mwenyewe.

5Je! Utavikazia macho vile ambavyo si kitu?

Maana bila shaka mali hujifanyia mabawa,

Kama tai arukaye mbinguni.

6Usile mkate wa mtu mwenye husuda;[#Zab 141:4; Kum 15:9; Mt 20:15; Mk 7:22]

Wala usivitamani vyakula vyake vya anasa;

7Maana aonavyo nafsini mwake, ndivyo alivyo.

Akuambia, Haya, kula, kunywa;

Lakini moyo wake hauwi pamoja nawe.

8Tonge lile ulilokula utalitapika,

Na maneno yako matamu yatakupotea.

9Usiseme masikioni mwa mpumbavu;[#Mt 7:6]

Maana atadharau hekima ya maneno yako.

10Usiiondoe alama ya mpaka wa zamani;

Wala usiingie katika mashamba ya yatima;

11Kwa sababu mkombozi wao ana nguvu;[#Ayu 31:21; Yer 50:34]

Atawatetea juu yako.

12Elekeza moyo wako kusikiliza mafundisho;

Tega masikio yako kusikia maneno ya maarifa.

13Usimnyime mtoto wako mapigo;

Maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa.

14Utampiga kwa fimbo,[#1 Kor 5:5]

Na kumwokoa nafsi yake na Kuzimu.

15Mwanangu, kama moyo wako una hekima,

Moyo wangu utafurahi, naam, moyo wangu;

16Naam, viuno vyangu vitafurahi,

Midomo yako inenapo maneno mema.

17Moyo wako usiwahusudu wenye dhambi;

Bali mche BWANA mchana kutwa;

18Maana bila shaka iko thawabu;[#Lk 16:25]

Na tumaini lako halitabatilika.

19Sikia, mwanangu, uwe na hekima,

Na kuuongoza moyo wako katika njia njema.

20Usiwe miongoni mwao wanywao mvinyo;[#Isa 5:22; Mt 24:49; Lk 21:34; Rum 13:13; Efe 5:18]

Miongoni mwao walao nyama kwa pupa.

21Kwa maana mlevi na mlafi huingia umaskini,

Na utepetevu humvika mtu nguo mbovu.

22Msikilize baba yako aliyekuzaa,[#Efe 6:1]

Wala usimdharau mama yako akiwa mzee.

23Inunue kweli, wala usiiuze;[#Mt 13:44]

Naam, hekima, na mafundisho, na ufahamu.

24Baba yake mwenye haki atashangilia;

Naye amzaaye mtoto mwenye hekima atamfurahia.

25Na wafurahi baba yako na mama yako;

Na afurahi aliyekuzaa.

26Mwanangu, nipe moyo wako;

Macho yako yapendezwe na njia zangu.

27Kwa maana kahaba ni shimo refu;

Na malaya ni mtego wa shimo jembamba.

28Naam, huotea kama mnyang'anyi;

Huwaongeza wenye hila katika wanadamu.

29Ni nani apigaye, Yowe? Ni nani aliaye, Ole?[#1 Fal 20:16; Mit 20:1; Isa 5:11; Nah 1:10; Mt 24:49,50; Efe 5:18]

Ni nani mwenye ugomvi? Ni nani mwenye mguno?

Ni nani aliye na majeraha yasiyo na sababu?

Ni nani aliye na macho mekundu?

30Ni wale wakaao sana kwenye mvinyo;

Waendao kutafuta divai iliyochanganyika.

31Usiutazame mvinyo iwapo ni mwekundu;

uitiapo bilauri rangi yake, ushukapo taratibu;

32Mwisho wake huuma kama nyoka;

Huchoma kama fira.

33Macho yako yataona mambo mageni;

Na moyo wako utatoa yaliyopotoka.

34Naam, utakuwa kama alalaye katikati ya bahari;

Au kama yeye asinziaye juu ya mlingoti.

35Utasema, Wamenichapa wala sikuumia;[#Mit 27:22; Yer 5:3; Kum 29:19; Isa 56:12; 2 Pet 2:22]

Wamenipiga wala sina habari;

Nitaamka lini, nitazidi kuitafuta tena.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya