Zaburi 28

Zaburi 28

Zaburi 28

Kuomba msaada

1Ninakuita wewe, Ee Bwana , Mwamba wangu;

usikatae kunisikiliza.

Kwa sababu ukinyamaza

nitafanana na walioshuka shimoni.

2Sikia kilio changu nikikuomba unihurumie,

ninapokuita ili unisaidie,

ninapoinua mikono yangu kuelekea

Patakatifu pa Patakatifu pako.

3Usiniburute pamoja na waovu,

pamoja na hao watendao mabaya,

ambao huzungumza na majirani zao maneno mazuri,

lakini mioyoni mwao wameficha chuki.

4Walipe sawasawa na matendo yao,

sawasawa na matendo yao maovu;

walipe sawasawa na kazi za mikono yao,

uwalipe wanavyostahili.

5Kwa kuwa hawaheshimu kazi za Bwana ,

na yale ambayo mikono yake imetenda,

atawabomoa na kamwe

hatawajenga tena.

6Ahimidiwe Bwana ,

kwa maana amesikia kilio changu

nikimwomba anihurumie.

7Bwana ni nguvu zangu na ngao yangu,

moyo wangu umemtumaini yeye,

nami nimesaidiwa.

Moyo wangu unarukaruka kwa furaha

nami nitamshukuru kwa wimbo.

8Bwana ni nguvu ya watu wake,

ngome ya wokovu kwa mpakwa mafuta wake.

9Waokoe watu wako na uubariki urithi wako;

uwe mchungaji wao na uwabebe milele.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.