Zaburi 52

Zaburi 52

Zaburi 52

Hukumu ya Mungu

1Ewe jitu, mbona unajivunia ubaya?

Kwa nini unajivuna mchana kutwa,

wewe ambaye ni fedheha mbele za Mungu?

2Ulimi wako hupanga mashauri mabaya ya maangamizi.

Ni kama wembe mkali, ninyi mnaofanya hila.

3Unapenda mabaya kuliko mema,

uongo kuliko kusema kweli.

4Unapenda kila neno lenye kudhuru,

ewe ulimi wenye hila!

5Hakika Mungu atakushusha chini

kwa maangamizi ya milele:

atakunyakua na kukuondoa kwa nguvu

kutoka hema lako,

atakungʼoa kutoka nchi ya walio hai.

6Wenye haki wataona na kuogopa;

watamcheka, wakisema,

7“Huyu ni yule mtu ambaye

hakumfanya Mungu kuwa ngome yake,

bali alitumainia wingi wa utajiri wake,

na akawa hodari kwa kuwaangamiza wengine!”

Neema ya Mungu

8Lakini mimi ni kama mti wa mzeituni

unaostawi katika nyumba ya Mungu,

nautegemea upendo wa Mungu usiokoma

milele na milele.

9Nitakusifu milele kwa yale uliyoyatenda,

nitatumaini jina lako, kwa kuwa jina lako ni jema.

Nitakusifu mbele ya watakatifu wako.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.