Isaya 47

Isaya 47

Hukumu dhidi ya Babuloni

1“Teremka uketi mavumbini[#Taz Isa 13:1–14:23; Yer 50:1–51:64]

ewe Babuloni binti mzuri!

Keti chini pasipo kiti cha enzi

ewe binti wa Wakaldayo!

Tokea sasa hutaitwa tena mwororo wala nadhifu.

2Twaa mawe ya kusagia, usage unga kama mtumwa!

Vua utaji wako, ukavue na mavazi yako!

Pandishia vazi lako miguuni, ukavuke mito.

3Watu watauona uchi wako;

naam, wataiona aibu yako.

Mimi nitalipiza kisasi,

wala sitamhurumia yeyote.”

4Mkombozi wetu ndiye Mtakatifu wa Israeli;

Mwenyezi-Mungu wa majeshi ndilo jina lake.

5Mwenyezi-Mungu asema:

“Ewe taifa la Wakaldayo

lililo kama binti mzuri,

keti kimya na kutokomea gizani.

Maana umepoteza hadhi yako

ya kuwa bimkubwa wa falme.

6Niliwakasirikia watu wangu Israeli,

nikawafanya watu wangu kuwa haramu.

Niliwatia mikononi mwako,

nawe hukuwaonea huruma;

na wazee uliwatwisha nira nzito mno.

7Ulijisemea moyoni: ‘Nitakuwa malkia milele’,

nawe hukuyatafakari mambo yanayotokea,

wala kufikiri mwisho wake.

8“Sasa, basi, sikiliza ewe mpenda anasa,[#Taz Ufu 18:7-8]

wewe unayedhani kuwa u salama,

na kujisemea: ‘Ni mimi tu,

na hakuna mwingine isipokuwa mimi.

Kamwe sitakuwa mjane,

wala sitafiwa na wanangu.’

9Haya yote mawili yatakupata,

ghafla, katika siku moja:

Kupoteza watoto wako na kuwa mjane,

ijapokuwa una wingi wa uchawi wako,

na nguvu nyingi za uganga wako.

10“Ulijiona salama katika uovu wako;

ukajisemea, ‘Hakuna mtu anayeniona.’

Hekima na elimu yako vilikupotosha,

ukajisemea moyoni mwako, ‘Mimi ndiye;

hakuna mwingine anayenishinda.’

11Lakini maafa yatakupata

ambayo hutaweza kujiepusha nayo.

Balaa litakukumba

ambalo hutaweza kulipinga;

maangamizi yatakujia ghafla

ambayo hujapata kamwe kuyaona.

12Endelea basi na uganga wako,

tegemea wingi wa uchawi wako.

Wewe uliyapania hayo tangu ujana wako

ukitumainia kwamba utafanikiwa

au kusababisha kitisho kwa watu!

13Wewe umejichosha bure na washauri wako.

Basi, na wajitokeze hao wanajimu wakuokoe!

Wao huzigawa mbingu sehemusehemu,

huzichunguza nyota

na kubashiri kila mwezi yatakayokupata.

14“Kumbuka, wao ni kama mabua makavu:

Moto utayateketezea mbali!

Hawawezi hata kujiokoa wenyewe

mbali na ukali wa moto huo.

Moto huo si wa kujipatia joto,

huo si moto wa kuota!

15Ndivyo watakavyokuwa hao uliowategemea hivyo,

hao uliojishughulisha nao tangu ujana wako.

Watatangatanga kila mmoja njia yake;

hakuna hata mmoja atakayeweza kukuokoa.”

Swahili Common Language DC Bible: Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki © Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya, 1995, 2001. Haki zote zimehifadhiwa.  
Published by: Bible Society of Tanzania