Warumi 12

Warumi 12

Maisha mapya katika Kristo

1Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.[#Rum 6:11,13; 1 Pet 2:5; Yn 4:24]

2Wala msifuate kanuni za dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.[#Efe 4:23; 5:10,17; Rum 1:28; Gal 1:4]

3Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinuie makuu kupita ilivyompasa kunuia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani.[#1 Kor 12:11; Efe 4:7]

4Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja;[#1 Kor 12:12]

5Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake.[#1 Kor 12:27; Efe 4:25]

6Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema tuliyopewa; ikiwa ni unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani;[#1 Kor 12:4-11]

7ikiwa ni huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake;[#1 Pet 4:10,11]

8mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; msimamizi, na asimamie kwa bidii; anayerehemu, na arehemu kwa furaha.[#Mt 6:3; 2 Kor 8:2; 9:7]

Sifa za Mkristo

9Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkilishika lililo jema.[#1 Pet 1:22; 1 Tim 1:5; Amo 5:15]

10Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu;[#2 Pet 1:7; Flp 2:3]

11kwa bidii, bila kulegea; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia Bwana;[#Ufu 3:15; Mdo 18:25]

12kwa tumaini, mkifurahi; katika dhiki, mkisubiri; mkidumu katika kusali;[#1 The 5:17]

13kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni mkijitahidi.[#Ebr 13:2]

14Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani.[#Mt 5:44; Lk 6:28; Mdo 7:59; 1 Kor 4:12]

15Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao.[#Zab 35:13]

16Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinuie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili.[#Mit 3:7; Rum 15:5; 11:20]

17Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote.[#Isa 5:21; 1 The 5:15]

18Ikiwezekana, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.[#Mk 9:50; Ebr 12:14]

19Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana.[#Kum 32:35; Law 19:18; Mt 5:39; 2 The 1:6,7; Rum 13:4; Ebr 10:30]

20Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.[#Mit 25:21-22; Mt 5:44]

21Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya