Zaburi 20

Zaburi 20

Kuomba ushindi

1Mwenyezi-Mungu akujibu uwapo taabuni;

jina la Mungu wa Yakobo likulinde.

2Akupelekee msaada kutoka hekaluni mwake;

akutegemeze kutoka mlima Siyoni.

3Azikumbuke sadaka zako zote;

azikubali tambiko zako za kuteketezwa.

4Akujalie unayotamani moyoni mwako,

aifanikishe mipango yako yote.

5Tutashangilia kwa ajili ya ushindi wako;

tutatweka bendera kulitukuza jina la Mungu wetu.

Mwenyezi-Mungu akutimizie maombi yako yote!

6Najua Mwenyezi-Mungu atamsaidia mfalme aliyemteua,

atamjibu kutoka patakatifu pake mbinguni;

kwa mkono wake wa kulia atamjalia ushindi mkubwa.

7Wengine hujigamba kwa magari ya vita;

wengine hujigamba kwa farasi wao.

Lakini sisi twajivunia Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.

8Hao watajikwaa na kuanguka;

lakini sisi tutainuka na kusimama imara.

9Umjalie mfalme ushindi, ee Mwenyezi-Mungu;

utujibu wakati tunapokuomba.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania