The chat will start when you send the first message.
1Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Mwenyezi-Mungu:[#30:1-9 Huduma ya Yeremia haikuhusu tu kung'oa na kuangamiza bali pia kupanda na kujenga (taz Yer 1:10). Katika baadhi ya sura zilizotangulia, hapa na pale tunakuta tangazo la wokovu Yer 3:4-17; 23:3-4, na ile barua kwa wahamishwa (Yer 29:10) ilitangaza mwisho wa uhamisho na kurudi kwa wahamishwa. Lakini sasa, ahadi hizo za kuokolewa na kurekebishwa zinaendelezwa zaidi katika sehemu ya kitabu cha Yeremia ijulikanayo kama: “Kitabu cha Faraja” (sura 30—33). Katika sehemu hii, nabii anaendelea na ujumbe wa Mungu katika mtindo wa kishairi, na maandishi ya kawaida yanatumiwa pale ambapo yahusu vitendo vya ishara (Taz Yer 13:1-11) ili kuwapasha watu wa Mungu ujumbe wa matumaini.]
2“Mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema hivi: Yaandike katika kitabu maneno yote niliyokuambia.[#30:2 Rejea Yer 36:2,4,28,32.]
3Maana siku zaja ambapo nitawarudishia fanaka zao watu wangu wa Israeli na Yuda na kuwarudisha katika nchi niliyowapa wazee wao, nao wataimiliki. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”[#30:3 Msemo wa kawaida katika kitabu cha Kumbukumbu la Sheria. Rejea Kumb 6:18,23; 7:8; 8:1; 10:11; 11:9,21.]
4Haya ndiyo mambo aliyosema Mwenyezi-Mungu kuhusu watu wa Israeli na Yuda:
5“Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Kumesikika kilio cha hofu
sauti ya kutisha wala si ya amani.
6Jiulizeni sasa na kufahamu:
Je, mwanamume aweza kujifungua mtoto?
Mbona basi, namwona kila mwanamume
amejishika kiunoni kama mwanamke mwenye utungu
na nyuso zao zimegeuka rangi?
7Kweli, siku hiyo ni kubwa,[#30:7 Dokezo juu ya siku ya Bwana (rejea Yoe 2:1,11; Sef 1:14; Ufu 6:17). Nabii Amosi alisema juu ya siku hiyo kama siku ya giza na sio ya mwanga (Amo 5:18). Yeremia naye anasema kuhusu siku hiyo kuwa ya upendo wa Mwenyezi-Mungu ambao anaponya majeraha ya watu wake (Yer 30:17) na kuwakusanya miongoni mwa mataifa na kuwawezesha kurudi katika nchi ya wazee wao (32:8).]
hakuna nyingine kama hiyo;
ni siku ya huzuni kwa watu wa Yakobo;
hata hivyo, wataokolewa humo.
8“Siku hiyo itakapofika, nasema mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, nitaivunja nira iliyo shingoni mwao na kukata minyororo yao.
9Nao hawatakuwa tena watumwa wa wageni, bali watanitumikia mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, na mfalme wa ukoo wa Daudi ambaye nitawateulia.
10“Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Usiogope ee Yakobo mtumishi wangu,
wala usifadhaike, ee Israeli;
maana nitakuokoa huko mbali uliko,
na wazawa wako kutoka uhamishoni.
Utarudi na kuishi kwa amani,
wala hakuna mtu atakayekuogopesha.
11Maana mimi niko pamoja nawe, kukuokoa.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
Nitayaangamiza kabisa mataifa yote,
ambayo nilikutawanya kati yao;
lakini wewe sitakuangamiza kabisa.
Nitakuadhibu kadiri unavyostahili
wala sitakuacha uende bila kukuadhibu.
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
12“Mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi:
Majeraha yako hayaponyeki,
vidonda vyako havitibiki.
13Hakuna atakayeshughulikia kisa chako,
jeraha lako halina dawa,
wewe hutaponyeshwa.
14Wapenzi wako wote wamekusahau;[#30:14 Taz Yer 22:20 maelezo.]
hawajali chochote juu yako,
nimekupiga pigo la adui;
umeadhibiwa bila huruma,
kwa kuwa kosa lako ni kubwa,
dhambi zako ni nyingi mno.
15Mbona unalia juu ya jeraha lako?
Maumivu yako hayaponyeki.
Nimekutendea hayo yote,
kwa sababu kosa lako ni kubwa,
dhambi zako ni nyingi mno.
16Lakini wote wanaokuangamiza, wataangamizwa,
na maadui zako wote watachukuliwa uhamishoni;
wanaokuteka nyara, watatekwa nyara,
wanaokuwinda nitawawinda.
17“Nitakurudishia afya yako,
na madonda yako nitayaponya,
japo wamekuita ‘Aliyetupwa’,
‘Mji Siyoni usio na wa kuutunza!’”
18Mwenyezi-Mungu asema hivi:
“Nitazirudisha tena fanaka za maskani ya Yakobo,
na kuyaonea huruma makao yake;
mji utajengwa upya juu ya magofu yake,
na ikulu ya mfalme itasimama pale ilipokuwa.
19Humo zitatoka nyimbo za shukrani
na sauti za wale wanaosherehekea.
Nitawaongeza na wala hawatakuwa wachache;
nitawafanya waheshimiwe wala hawatadharauliwa.
20Watoto wao watakuwa kama walivyokuwa zamani,
jumuiya yao itaimarika mbele yangu,
nami nitawaadhibu wote wanaowakandamiza.
21Kiongozi wao atakuwa mmoja wao,
mtawala wao atatokea miongoni mwao.
Nitamleta karibu naye atanikaribia;
maana, nani anayethubutu kunikaribia kwa nguvu zake?
Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.
22Nanyi mtakuwa watu wangu,
nami nitakuwa Mungu wenu.”
23Tazama, dhoruba kali kutoka kwa Mwenyezi-Mungu!
Ghadhabu imezuka,
kimbunga cha tufani
kitamlipukia mtu mwovu kichwani.
24Hasira ya Mwenyezi-Mungu haitarudi nyuma,
mpaka atakapotekeleza na kukamilisha
matakwa ya moyo wake.
Siku zijazo mtayaelewa vema mambo hayo.