The chat will start when you send the first message.
1“Imba, ewe mwanamke tasa,
wewe ambaye kamwe hukuzaa mtoto;
paza sauti kwa kuimba, piga kelele kwa furaha,
wewe ambaye kamwe hukupata uchungu;
kwa sababu watoto wa mwanamke aliyeachwa ukiwa ni wengi
kuliko wa mwanamke mwenye mume,”
asema Bwana .
2“Panua mahali pa hema lako,
tandaza mapazia ya hema lako uyaeneze mbali,
wala usiyazuie;
ongeza urefu wa kamba zako,
imarisha vigingi vyako.
3Kwa maana utaenea upande wa kuume
na upande wa kushoto;
wazao wako watayamiliki mataifa
na kukaa katika miji yao iliyoachwa ukiwa.
4“Usiogope, wewe hutaaibika.
Usiogope aibu, wewe hutaaibishwa.
Wewe utasahau aibu ya ujana wako,
wala hutakumbuka tena mashutumu ya ujane wako.
5Kwa maana Muumba wako ndiye mume wako,
Bwana wa majeshi ndilo jina lake,
yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli ni Mkombozi wako,
yeye anaitwa Mungu wa dunia yote.
6Bwana atakuita urudi
kana kwamba ulikuwa mke aliyeachwa na kuhuzunishwa rohoni;
kama mke aliyeolewa bado angali kijana
na kukataliwa,” asema Mungu wako.
7“Kwa kitambo kidogo nilikuacha,
lakini kwa huruma nyingi nitakurudisha.
8Katika ukali wa hasira
nilikuficha uso wangu kwa kitambo,
lakini kwa fadhili za milele
nitakuwa na huruma juu yako,”
asema Bwana Mkombozi wako.
9“Kwangu mimi jambo hili ni kama siku za Nuhu,
nilipoapa kuwa maji ya Nuhu kamwe hayatafunika tena dunia.
Hivyo sasa nimeapa sitawakasirikia ninyi,
kamwe sitawakemea tena.
10Ijapotikisika milima, na vilima viondolewe,
hata hivyo upendo wangu usiokoma kwenu hautatikisika,
wala agano langu la amani halitaondolewa,”
asema Bwana , mwenye huruma juu yenu.
11“Ewe mji uliyeteswa, uliyepigwa kwa dhoruba
na usiyetulizwa,
nitakujenga kwa almasi,
nitaweka misingi yako
kwa yakuti samawi.
12Nitafanya minara yako ya akiki,
malango yako kwa vito vingʼaavyo,
nazo kuta zako zote za vito vya thamani.
13Watoto wako wote watafundishwa na Bwana ,
nayo amani ya watoto wako itakuwa kuu.
14Kwa haki utathibitika:
Kuonewa kutakuwa mbali nawe;
hutaogopa chochote.
Hofu itakuwa mbali nawe;
haitakukaribia wewe.
15Kama mtu yeyote akikushambulia,
haitakuwa kwa ruhusa yangu;
yeyote akushambuliaye
atajisalimisha kwako.
16“Tazama, ni mimi niliyemuumba mhunzi,
yeye afukutaye makaa kuwa moto,
na kutengeneza silaha inayofaa kwa kazi yake.
Tena ni mimi niliyemwambia mharibu
kufanya uharibifu mwingi.
17Hakuna silaha itakayofanyizwa dhidi yako
itakayofanikiwa,
nawe utauthibitisha kuwa mwongo
kila ulimi utakaokushtaki.
Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana
na hii ndiyo haki yao inayotoka kwangu,”
asema Bwana .