Isaya 58

Isaya 58

Mfungo wa kweli

1“Piga kelele, usizuie.

Paza sauti yako kama tarumbeta.

Watangazieni watu wangu uasi wao,

na kwa nyumba ya Yakobo dhambi zao.

2Kwa maana kila siku hunitafuta,

wanaonekana kutaka kujua njia zangu,

kana kwamba walikuwa taifa linalotenda lililo sawa,

na ambalo halijaziacha amri za Mungu wake.

Hutaka kwangu maamuzi ya haki,

nao hutamani Mungu awakaribie.

3Wao husema, ‘Mbona tumefunga, nawe hujaona?

Mbona tumejinyenyekeza, nawe huangalii?’

“Lakini katika siku ya kufunga kwenu, mnafanya mnavyotaka

na kuwadhulumu wafanyakazi wenu wote.

4Kufunga kwenu huishia kwenye magomvi na mapigano,

na kupigana ninyi kwa ninyi kwa ngumi za uovu.

Hamwezi kufunga kama mnavyofanya leo

na kutazamia sauti zenu kusikiwa huko juu.

5Je, hii ndiyo aina ya mfungo niliouchagua,

siku moja tu ya mtu kujinyenyekeza?

Je, ni kwa kuinamisha kichwa chini kama tete,

na kwa kujilaza juu ya gunia na majivu?

Je, huo ndio mnaouita mfungo,

siku iliyokubalika kwa Bwana ?

6“Je, hii si ndiyo aina ya mfungo niliyoichagua:

kufungua minyororo ya udhalimu,

na kufungua kamba za nira,

kuwaweka huru waliodhulumiwa,

na kuvunja kila nira?

7Je, sio kushirikiana chakula chako na wenye njaa

na kuwapatia maskini wasiokuwa na makao hifadhi,

unapomwona aliye uchi, umvike,

wala si kumkimbia mtu wa mwili wako

na damu yako mwenyewe?

8Ndipo nuru yako itajitokeza kama mapambazuko

na uponyaji wako utatokea upesi;

ndipo haki yako itakapokutangulia mbele yako,

na utukufu wa Bwana utakuwa mlinzi nyuma yako.

9Ndipo utaita, naye Bwana atajibu,

utalia kuomba msaada,

naye atasema: Mimi hapa.

“Ukiiondoa nira ya udhalimu,

na kunyoosha kidole na kuzungumza maovu,

10nanyi mkimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi zenu

na kutosheleza mahitaji ya waliodhulumiwa,

ndipo nuru yenu itangʼaa gizani,

nao usiku wenu utakuwa kama adhuhuri.

11Bwana atakuongoza siku zote,

atayatosheleza mahitaji yako katika nchi kame,

naye ataitia nguvu mifupa yako.

Utakuwa kama bustani iliyonyweshwa vizuri,

kama chemchemi ambayo maji yake hayakauki kamwe.

12Watu wako watajenga tena magofu ya zamani

na kuinua misingi ya kale;

utaitwa Mwenye Kukarabati Kuta Zilizobomoka,

Mwenye Kurejesha Barabara za Makao.

13“Ukitunza miguu yako isivunje Sabato,

na kutokufanya kama vile upendavyo katika siku yangu takatifu,

ukiita Sabato siku ya furaha

na siku takatifu ya Bwana ya kuheshimiwa,

kama utaiheshimu kwa kutoenenda

katika njia zako mwenyewe,

na kutokufanya yakupendezayo

au kusema maneno ya upuzi,

14ndipo utakapojipatia furaha yako katika Bwana ,

nami nitakufanya upande juu ya miinuko ya nchi

na kusherehekea urithi wa Yakobo baba yako.”

Kinywa cha Bwana kimenena haya.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.