Zaburi 42

Zaburi 42

Kitabu cha Pili

Zaburi 42

Maombi ya mtu aliye uhamishoni

1Kama ayala anavyoonea shauku vijito vya maji,

ndivyo nafsi yangu inavyokuonea shauku, Ee Mungu.

2Nafsi yangu inamwonea Mungu kiu, Mungu aliye hai.

Ni lini nitaweza kwenda kukutana na Mungu?

3Machozi yangu yamekuwa chakula changu

usiku na mchana,

huku watu wakiniambia mchana kutwa,

“Yuko wapi Mungu wako?”

4Mambo haya nayakumbuka

ninapoimimina nafsi yangu:

Jinsi nilivyokuwa nikienda na umati wa watu,

nikiongoza maandamano kuelekea kwenye nyumba ya Mungu,

kwa kelele za shangwe na za shukrani

katikati ya umati wa watu waliosherehekea.

5Ee nafsi yangu, kwa nini unasononeka?

Kwa nini unafadhaika hivyo ndani yangu?

Weka tumaini lako kwa Mungu,

kwa kuwa bado nitamsifu,

Mwokozi wangu na Mungu wangu.

6Nafsi yangu inasononeka ndani yangu;

kwa hiyo nitakukumbuka

kutoka nchi ya Yordani,

katika vilele vya Hermoni,

kutoka Mlima Mizari.

7Kilindi huita kilindi,

katika ngurumo za maporomoko ya maji yako;

mawimbi yako yote pamoja na viwimbi

vimepita juu yangu.

8Bwana huelekeza upendo wake mchana,

wimbo wake uko nami usiku:

maombi kwa Mungu wa uzima wangu.

9Ninamwambia Mungu Mwamba wangu,

“Kwa nini umenisahau?

Kwa nini niendelee kuomboleza,

nikiteswa na adui?”

10Mifupa yangu inateseka kwa maumivu makali

adui zangu wanaponidhihaki,

wakiniambia mchana kutwa,

“Yuko wapi Mungu wako?”

11Ee nafsi yangu, kwa nini unasononeka?

Kwa nini unafadhaika hivyo ndani yangu?

Weka tumaini lako kwa Mungu,

kwa kuwa bado nitamsifu,

Mwokozi wangu na Mungu wangu.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.