Zaburi 91

Zaburi 91

Zaburi 91

Mungu mlinzi wetu

1Yeye akaaye mahali pa salama pake Yeye Aliye Juu Sana,

atadumu katika uvuli wake Mwenyezi.

2Nitasema kumhusu Bwana , “Yeye ndiye kimbilio langu na ngome yangu,

Mungu wangu, ninayemtumaini.”

3Hakika yeye ataniokoa na mtego wa mwindaji,

na maradhi ya kuambukiza ya kuua.

4Atakufunika kwa manyoya yake,

chini ya mabawa yake utapata kimbilio,

uaminifu wake utakuwa ngao na kinga yako.

5Hutaogopa vitisho vya usiku,

wala mshale urukao mchana,

6wala maradhi ya kuambukiza

yanayonyemelea gizani,

wala tauni iharibuyo adhuhuri.

7Ijapo watu elfu wataangukia kando yako,

kumi elfu mkono wako wa kuume,

lakini haitakukaribia wewe.

8Utatazama tu kwa macho yako

na kuona adhabu ya waovu.

9Ukimfanya Aliye Juu Sana kuwa makao yako;

naam, Bwana ambaye ni kimbilio langu;

10basi hakuna madhara yatakayokupata wewe,

hakuna maafa yatalikaribia hema lako.

11Kwa kuwa atawaagiza malaika wake kwa ajili yako,

wakulinde katika njia zako zote.

12Watakuchukua mikononi mwao,

ili usijikwae mguu wako kwenye jiwe.

13Utawakanyaga simba na nyoka wakali,

simba mkubwa na nyoka utawaponda kwa miguu.

14Bwana asema, “Kwa kuwa ananipenda, nitamwokoa;

nitamlinda, kwa kuwa analikiri Jina langu.

15Ataniita, nami nitamjibu;

nitakuwa pamoja naye katika taabu,

nitamwokoa na kumheshimu.

16Kwa siku nyingi nitamshibisha

na kumwonesha wokovu wangu.”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.