Baruku 5

Baruku 5

1Ee Yerusalemu, vua nguo za matanga na huzuni,[#Isa 52:1; 61:3,10; Ufu 21:2]

Uvae uzuri wa utukufu utokao kwa Mungu milele.

2Jifunge nguo ya haki itokayo kwa Mungu,

Jipige kilemba kichwani cha utukufu wake Aliye wa Milele.

3Maana Mungu ataidhihirisha nuru yako duniani kote,

4Na jina lako litaitwa na Mungu daima,

Amani ya haki, na Utukufu wa utauwa.

5Ondoka, Ee Yerusalemu, usimame juu;

Tazama upande wa mashariki, uangalie.

Toka machweo ya jua hata mawio yake wanao wanakusanyika

Kwa neno lake Yeye Aliye Mtakatifu,

Wakifurahi kwa kuwa Mungu amewakumbuka.

6Waliondoka kwako kwa miguu, wakikokotwa na adui zao,

Lakini Mungu anawarejeza kwako wameinuliwa juu kwa heshima

Kama katika kiti cha enzi.

7Maana kwa maagizo ya Mungu

Kila kilima kirefu kitashushwa,

Na milima ya milele.

Na mabonde yote yatajazwa,

Hata nchi iwe sawa,

Ili Israeli aende salama

Katika utukufu wa Mungu.

8Nayo misitu, na miti yote itoayo harufu nzuri,

Imemtia Israeli kivuli kwa amri ya Mungu;

9Kwa kuwa Mungu atamwongoza Israeli kwa furaha

Katika mwangaza wa utukufu wake,

Kwa ile rehema na haki itokayo kwake.

The Holy Bible in Kiswahili, Revised Union Version © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 2013. 
Published by: Bible Society of Tanzania