The chat will start when you send the first message.
1BWANA asema hivi, Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni mahali pa kuweka miguu yangu; mtanijengea nyumba ya namna gani? Na mahali pangu pa kupumzikia ni mahali gani?[#1 Nya 28:2; 2 Nya 6:18; Zab 11:4; Mdo 7:48,49; Mt 5:34-35; 23:22]
2Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema BWANA; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.[#Zab 34:18; Ezr 9:4; Zab 119:120,161; Mit 28:14]
3Yeye achinjaye ng'ombe ni kama yeye amwuaye mtu; na yeye atoaye dhabihu ya mwana-kondoo ni kama yeye avunjaye shingo ya mbwa; na yeye atoaye matoleo ni kama yeye atoaye damu ya nguruwe; na yeye afukizaye uvumba ni kama yeye abarikiye sanamu; naam, wamezichagua njia zao wenyewe, na nafsi zao zafurahia machukizo yao.
4Mimi nami nitachagua mapigo yao, nitaleta hofu zao juu yao; kwa sababu nilipoita, hawakuitika; na niliponena, hawakusikia; bali walifanya yaliyo maovu machoni pangu, na kuyachagua nisiyoyafurahia.[#Mit 1:24]
5Lisikilizeni neno la BWANA, ninyi mtetemekao kwa sababu ya neno lake; Ndugu zenu wawachukiao ninyi, waliowatupa kwa ajili ya jina langu, wamesema, Na atukuzwe BWANA, tupate kuiona furaha yenu; lakini watatahayarika.[#Yn 15:18; Mt 24:9; Isa 5:19; 2 The 1:10; Tit 2:13]
6Sauti ya fujo itokayo mjini!
Sauti itokayo hekaluni!
Sauti ya BWANA awalipaye adui zake adhabu!
7Kabla hajawa na uchungu alizaa;[#Ufu 12:5]
Kabla maumivu yake hayajampata,
Alizaa mtoto wa kiume.
8Ni nani aliyesikia neno kama hili?
Ni nani aliyeona mambo kama haya?
Je! Nchi yaweza kuzaliwa kwa siku moja?
Taifa laweza kuzaliwa mara?
Maana Sayuni, mara alipopata uchungu,
Alizaa watoto wake.
9Je! Mimi nilete wana karibu na kuzaliwa, nisizalishe? Asema BWANA; mimi nizalishaye, je! Nilifunge tumbo? Asema Mungu wako.
10Furahini pamoja na Yerusalemu, shangilieni kwa ajili yake, ninyi nyote mmpendao; furahini pamoja naye kwa furaha, ninyi nyote mliao kwa ajili yake;
11mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa ya faraja zake, mpate kukama, na kufurahiwa kwa wingi wa utukufu wake.
12Maana BWANA asema hivi, Tazama, nitamwelekezea amani kama mto, na utukufu wa mataifa kama kijito kifurikacho, nanyi mtapata kunyonya; mtabebwa; na juu ya magoti mtabembelezwa.[#Isa 48:18; 49:22; 60:4,5,16]
13Mfano wa mtu ambaye mama yake amfariji, ndivyo nitakavyowafariji ninyi; nanyi mtafarijiwa katika Yerusalemu.
14Nanyi mtaona, na mioyo yenu itafurahi, na mifupa yenu itasitawi kama majani mabichi; na mkono wa BWANA utajulikana, uwaelekeao watumishi wake, naye atawaonea adui zake ghadhabu.[#Eze 37:1]
15Maana BWANA atakuja na moto, na magari yake ya vita kama upepo wa kisulisuli; ili atoe malipo ya ghadhabu yake kwa moto uwakao, na maonyo yake kwa miali ya moto.[#Isa 9:5; 2 The 1:8]
16Kwa maana BWANA atatoa hukumu kwa watu wote kwa moto, na kwa upanga wake, nao watakaouawa na BWANA watakuwa wengi.[#Isa 27:1]
17Watu wale wajitakasao, na kujisafisha katika bustani, nyuma yake aliye katikati; wakila nyama ya nguruwe, na machukizo, na panya; watakoma pamoja, asema BWANA.[#Isa 65:3,4]
18Nami nayajua matendo yao na mawazo yao; wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu.[#Ufu 2:2; Ebr 4:13]
19Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, Tarshishi, na Puli, na Ludi, wavutao upinde, kwa Tubali na Yavani, visiwa vilivyo mbali; watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa.[#Lk 2:34; Mal 1:11]
20Nao watawaleta ndugu zenu wote kutoka mataifa yote, kuwa sadaka kwa BWANA, juu ya farasi, na katika magari, na katika machela, na juu ya nyumbu, na juu ya wanyama wepesi, mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu, asema BWANA; kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka yao nyumbani kwa BWANA katika chombo safi.[#Rum 12:1; 15:16]
21Na baadhi ya hao nitawatwaa kuwa makuhani na Walawi, asema BWANA.[#Kut 19:6; Isa 61:6]
22Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema BWANA, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.[#Isa 65:17; 2 Pet 3:13; Ufu 21:1]
23Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema BWANA.[#Zek 14:16; Zab 65:2]
24Nao watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.[#Mk 9:48]