Hesabu 23

Hesabu 23

1Balaamu akamwambia Balaki, Nijengee hapa madhabahu saba, ukaniandalie hapa ng'ombe dume saba, na kondoo dume saba.

2Balaki akafanya kama Balaamu alivyonena. Balaki na Balaamu wakatoa sadaka, ng'ombe dume mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.

3Balaamu akamwambia Balaki, Simama karibu na sadaka yako, nami nitakwenda, labda BWANA atakuja kuonana nami; na lolote atakalonionesha nitakuambia. Akaenda hadi mahali peupe juu ya kilima.

4Mungu akakutana na Balaamu; naye Balaamu akamwambia, Nimetengeneza madhabahu saba, nami nimetoa sadaka ng'ombe dume mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.

5BWANA akatia neno katika kinywa chake Balaamu, akasema, Umrudie Balaki; ukaseme maneno haya.[#Kum 18:18; Yer 1:9]

6Akarudi kwake, na tazama, amesimama karibu na sadaka yake ya kuteketezwa, yeye na wakuu wote wa Moabu pamoja naye.

7Akatunga mithali yake, akasema,[#Ayu 27:21; Zab 78:2; Eze 17:2; 20:49; Mik 2:4; Hab 2:6; Mt 13:35; Mwa 10:22; 1 Sam 17:10]

Balaki amenileta kutoka Aramu,

Mfalme wa Moabu kutoka milima ya mashariki,

Njoo! Unilaanie Yakobo,

Njoo! Unishutumie Israeli.

8Nimlaanije, yeye ambaye Mungu hakumlaani?[#Mit 21:30; Isa 47:12]

Nimshutumuje, yeye ambaye BWANA hakumshutumu?

9Kutoka kilele cha majabali namwona;[#Law 20:24; Kum 33:28; 1 Fal 8:53; Ezr 9:2; Efe 2:14]

Na kutoka milimani namtazama;

Angalia, ni watu wakaao peke yao,

Wala hawatahesabiwa pamoja na mataifa.

10Ni nani awezaye kufanya idadi ya mavumbi ya Yakobo,[#Mwa 22:17; Zab 116:15; Isa 57:1,2]

Au kuhesabu robo ya Israeli?

Na nife kifo chake mwenye haki,

Na mwisho wangu uwe mfano wa mwisho wake.

11Balaki akamwambia Balaamu, Umenitendea nini? Nimekuleta ili Uwalaani adui zangu, na tazama, umewabariki kabisa kabisa.[#Yos 24:10; Neh 13:2]

12Naye akajibu, akasema, Je! Hainipasi kuangalia, niseme neno lile BWANA atialo kinywani mwangu?

Aguzi la pili la Balaamu

13Balaki akamwambia, Haya! Njoo, tafadhali, hata mahali pengine, na kutoka huko utaweza kuwaona; utaona upande wa mwisho wao tu, wala hutawaona wote, ukanilaanie hao kutoka huko.

14Akamchukua mpaka shamba la Sofimu, hadi kilele cha Pisga, akajenga madhabahu saba, akatoa sadaka ng'ombe dume mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.[#Isa 1:10,11; Hos 12:11]

15Akamwambia Balaki, Simama hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa, nami nitaonana na BWANA kule.

16BWANA akaonana na Balaamu akatia neno kinywani mwake, akasema, Umrudie Balaki, ukaseme hivi.

17Akafika kwake, na tazama, amesimama karibu na sadaka yake ya kuteketezwa, na wakuu wa Moabu pamoja naye. Balaki akamwambia, BWANA amenena nini?[#1 Sam 3:17]

18Naye akatunga mithali yake, akasema,[#Amu 3:20]

Ondoka Balaki, ukasikilize;

Nisikilize, Ee mwana wa Sipori;

19Mungu si mtu, aseme uongo;[#1 Sam 15:29; Zab 102:26,27; Mal 3:6; Rum 11:29; Tit 1:2; Yak 1:17]

Wala si mwanadamu, ajute;

Iwapo amesema, hatalitenda?

Iwapo amenena, hatalitimiza?

20Tazama, nimepewa amri kubariki,[#Mwa 12:2; 22:17; Hes 22:12]

Yeye amebariki, nami siwezi kulitangua.

21Hakutazama uovu katika Yakobo,[#Yer 50:20; Hos 14:2-4; Mik 7:18-20; Rum 4:7; 6:14; 8:1; 2 Kor 5:19; Kut 13:21; 29:45,46; Zab 89:18; 97:1; 98:6; Isa 33:22; Lk 19:37,38]

Wala hakuona ukaidi katika Israeli.

BWANA, Mungu wake, yu pamoja naye,

Na sauti kuu ya mfalme iko katikati yao.

22Mungu amewaleta kutoka Misri,[#Kum 33:17]

Naye ana nguvu kama nguvu za nyati.

23Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo,[#Zab 31:19]

Wala hapana uganga juu ya Israeli.

Sasa habari za Yakobo na Israeli zitasemwa,

Ni mambo gani aliyoyatenda Mungu!

24Tazama, watu hawa wanaondoka kama simba jike,

Na kama simba anajiinua nafsi yake,

Hatalala hadi atakapokula mawindo,

Na kunywa damu yao waliouawa.

25Balaki akamwambia Balaamu, Basi usiwalaani kabisa, wala usiwabariki kabisa.

26Lakini Balaamu akajibu akamwambia Balaki, Je! Sikukuambia ya kwamba, Kila neno BWANA atakalolisema sina budi kulitenda?

27Kisha Balaki akamwambia Balaamu, Haya, njoo sasa, nikupeleke mahali pengine; labda Mungu ataridhia kwamba unilaanie watu hao huko.

28Basi Balaki akamchukua Balaamu akaenda naye mpaka kilele cha mlima Peori, mahali paelekeapo upande wa nyika iliyo chini yake.

29Balaamu akamwambia Balaki, Haya, unijengee hapa madhabahu saba, kisha uniandalie ng'ombe dume saba, na kondoo dume saba.[#2 Pet 2:16]

30Basi Balaki akafanya kama Balaamu alivyosema, akasongeza sadaka ng'ombe dume na kondoo dume juu ya kila madhabahu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya