Zaburi 86

Zaburi 86

Maombi ya kutaka msaada juu ya watesi

1Ee BWANA, utege sikio lako unijibu,

Maana mimi ni maskini na mhitaji.

2Unihifadhi nafsi yangu,

Maana mimi ni mcha Mungu.

Wewe uliye Mungu wangu,

Umwokoe mtumishi wako anayekutumaini.

3Wewe, Bwana, unifadhili,

Maana nakulilia Wewe mchana kutwa.

4Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako,

Maana nafsi yangu nakuinulia Wewe, Bwana.

5Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema,[#Zab 130:7-8; Yoe 2:13]

Umekuwa tayari kusamehe,

Na mwingi wa fadhili,

Kwa watu wote wakuitao.

6Ee BWANA, uyasikie maombi yangu;

Uisikilize sauti ya dua zangu.

7Siku ya mateso yangu nitakuita,

Kwa maana utaniitikia.

8Katikati ya miungu hakuna kama Wewe, Bwana,[#Kut 15:11; Kum 3:24; 1 Sam 2:2; 2 Sam 7:22; 1 Fal 8:23]

Wala matendo mfano wa matendo yako.

9Mataifa yote uliyoyaumba watakuja;[#Zab 95:6-7; Isa 43:7; Ufu 15:4]

Watakusujudia Wewe, Bwana,

Watalitukuza jina lako;

10Kwa kuwa ndiwe uliye mkuu,[#Kum 6:4; Isa 37:16; Mk 12:29; 1 Kor 8:4; Efe 4:6]

Wewe ndiwe mfanya miujiza,

Ndiwe Mungu peke yako.

11Ee BWANA, unifundishe njia yako;

Nitakwenda katika kweli yako;

Moyo wangu na ufurahi kulicha jina lako;

12Nitakusifu Wewe, Ee Bwana, Mungu wangu,

Kwa moyo wangu wote,

Nitalitukuza jina lako milele.

13Maana fadhili zako kwangu ni nyingi sana;[#Zab 56:13]

Umeiopoa nafsi yangu na kuzimu.

14Ee Mungu, wenye kiburi wamenishambulia;

Kundi la watu wakatili wanataka kuniua.

Wala hawakukuweka Wewe

Mbele ya macho yao.

15Lakini Wewe, Bwana,[#Kut 34:6; Hes 14:18; Neh 9:17; Yoe 2:13; Zab 103:8; 111:4]

U Mungu wa rehema na neema,

Mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli.

16Unielekee na kunifadhili mimi;

Mpe mtumishi wako nguvu zako,

Umwokoe mwana wa mjakazi wako.

17Unifanyie ishara ya wema,

Wanichukiao waione na kuaibishwa.

Kwa kuwa Wewe, BWANA,

Umenisaidia na kunifariji.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya