Zaburi 24

Zaburi 24

Mfalme Mkuu

1Dunia na vyote vilivyomo ni vyake Mwenyezi-Mungu;[#Taz 1Kor 10:26]

ulimwengu na wote waishio humo ni mali yake.

2Maana yeye aliweka misingi ya dunia juu ya bahari;

aliisimika imara juu ya mito ya maji.

3Nani atakayepanda mlima wa Mwenyezi-Mungu?

Nani atakayekaa katika hekalu lake takatifu?

4Ni mtu wa matendo mema na moyo safi,[#Taz Mat 5:8]

asiyeuelekeza moyo wake katika upuuzi,

wala kuapa kwa uongo.

5Mtu huyo atapokea baraka kwa Mwenyezi-Mungu,

na haki yake kwa Mungu mwokozi wake.

6Ndio hali ya kizazi cha watu wamtafutao yeye;

naam, watu wamtafutao Mungu wa Yakobo.

7Fungukeni enyi milango;

fungukeni enyi milango ya kale,

ili Mfalme mtukufu aingie.

8Ni nani huyo Mfalme mtukufu?

Ni Mwenyezi-Mungu, mwenye nguvu na uwezo;

Mwenyezi-Mungu, mwenye uwezo vitani.

9Fungukeni enyi malango,

fungukeni enyi milango ya kale,

ili Mfalme mtukufu aingie.

10Ni nani huyo Mfalme mtukufu?

Ni Mwenyezi-Mungu, wa majeshi,

yeye ndiye Mfalme mtukufu.

Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania