Zaburi 136

Zaburi 136

Wimbo wa shukrani

1Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

2Mshukuruni Mungu wa miungu;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

3Mshukuruni Bwana wa mabwana;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

4Ndiye peke yake atendaye makuu ya ajabu;[#136:4 Au, “miujiza mikubwa”.]

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

5Ndiye aliyeziumba mbingu kwa hekima;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

6Ndiye aliyeitengeneza nchi juu ya vilindi vya maji;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

7Ndiye aliyeumba jua, mwezi na nyota;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

8Jua liutawale mchana;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

9Mwezi na nyota vitawale usiku;[#136:5-9 Kuhusu hekima ya Mungu na kuumbwa ulimwengu taz Meth 3:19-20; 8:22-31; Yer 10:12.]

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

10Ndiye aliyewaua wazaliwa wa kwanza wa Misri;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

11Akawaondoa watu wa Israeli kutoka huko;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

12Kwa mkono wake wenye nguvu na enzi;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

13Ndiye aliyeigawa Bahari ya Shamu sehemu mbili;

kwa maana fadhili zake zadumu milele,

14akawapitisha watu wa Israeli humo;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

15Lakini akawazamisha humo Farao na jeshi lake;[#136:10-15 Mwanazaburi anakumbuka jinsi Mungu alivyowaokoa Waisraeli kutoka Misri na kuwaongoza salama kupita Bahari ya Shamu (Kut 12:29-42; 51:14).]

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

16Ndiye aliyewaongoza watu wake jangwani;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

17Ndiye aliyewapiga wafalme wenye nguvu;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

18Akawaua wafalme maarufu;

kwa maana fadhili zake zadumu milele;

19akamuua Sihoni, mfalme wa Waamori,

kwa maana fadhili zake zadumu milele;

20na Ogu, mfalme wa Bashani;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

21Akachukua nchi zao akawapa watu wake;

kwa maana fadhili zake zadumu milele;

22ziwe riziki ya Israeli, mtumishi wake;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

23Ndiye aliyetukumbuka wakati wa unyonge wetu;

kwa maana fadhili zake zadumu milele;

24akatuokoa kutoka maadui zetu;[#136:24 Maadui hapa wanaweza kuwa Wamisri ikiwa kuokolewa huko ni kutoka Misri; la sivyo ni kuokolewa kutoka uhamishoni Babuloni, tukio ambalo lilichukuliwa pia kama hali mpya ya “Kutoka” (137:1-3).]

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

25Ndiye akipaye kila kiumbe chenye uhai chakula;

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

26Mshukuruni Mungu wa mbinguni;

kwa maana fadhili zake zadumu milele!

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993 The Bible Society of Kenya 1993
Published by: Bible Society of Tanzania