Ayubu 14

Ayubu 14

Ayubu anaendelea

1“Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke

siku zake ni chache nazo zimejaa taabu.

2Huchanua kama ua kisha hunyauka;

huwa kama kivuli kipitacho upesi, wala hadumu.

3Je, unamwekea jicho lako mtu kama huyo?

Je, utamleta mbele yako katika hukumu?

4Ni nani awezaye kutoa kitu safi kutoka kitu najisi?

Hakuna awezaye!

5Siku za mwanadamu zimewekewa mpaka;

umekwisha kutangaza idadi ya miezi yake

na kuweka mpaka ambao hawezi kuuvuka.

6Hivyo angalia mbali umwache,

hadi awe amekamilisha muda wake

kama mtu aliyeajiriwa.

7“Kwa maana lipo tumaini kwa mti;

kama ukikatwa utachipuka tena,

nayo machipukizi yake mapya hayatakoma.

8Mizizi yake yaweza kuchakaa ardhini

na kisiki chake kufa udongoni,

9lakini kwa kupata dalili ya maji utachipua

na kutoa machipukizi kama mche.

10Lakini mwanadamu hufa, na huo ndio mwisho wake;

hutoa pumzi ya mwisho, naye hayuko tena!

11Kama vile maji yanavyotoweka katika bahari,

au mkondo wa mto ukaushwavyo na kuwa mkavu,

12ndivyo mwanadamu alalavyo chini asiamke;

hadi mbingu zitakapokuwa hazipo tena,

wanadamu hawataamka au kuamshwa

kutoka usingizi wao.

13“Laiti kama ungenificha kaburini,[#14:13 Kaburini maana yake ni Kuzimu ; kwa Kiebrania ni Sheol.]

na kunisitiri hadi hasira yako ipite!

Laiti ungeniwekea wakati,

na kisha ukanikumbuka!

14Je, kama mtu akifa, aweza kuishi tena?

Siku zote za kazi zangu ngumu

nitangojea kufanywa upya kwangu.

15Utaniita nami nitakuitika;

utakionea shauku kiumbe ambacho mikono yako ilikiumba.

16Hakika ndipo utakapozihesabu hatua zangu,

lakini hutazifuatia dhambi zangu.

17Makosa yangu yatatiwa muhuri kwenye mfuko,

nawe utazifunika dhambi zangu.

18“Lakini kama mlima umomonyokavyo na kufikichika

na kama vile mwamba uondolewavyo mahali pake,

19kama maji yamalizavyo mawe,

na mafuriko yachukuavyo udongo,

ndivyo unavyoharibu tegemeo la mwanadamu.

20Humshinda mara moja kwa daima, naye hutoweka;

waibadilisha sura yake na kumwondoa.

21Kama wanawe wakipewa heshima, yeye hafahamu;

kama wazao wake wakidharauliwa, yeye haoni.

22Yeye hasikii kingine isipokuwa maumivu ya mwili wake mwenyewe,

naye huomboleza kwa ajili yake mwenyewe.”

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.