Danieli 2

Danieli anaifumbua ndoto ya mfalme Nebukadinesari.

(Taz. Dan. 7.)

1Katika mwaka wa pili wa ufalme wake mfalme Nebukadinesari akaota ndoto, zikamhangaisha rohoni, kwa hiyo usingizi ukampotelea.

2Ndipo, mfalme alipoagiza kuwaita waandishi na waaguaji na waganga na Wakasidi, waje kumwambia mfalme maana ya ndoto zake.[#Yes. 47:12-13.]

3Wakaja, wakajipanga mbele yake mfalme. Mfalme akawaambia: Nimeota ndoto, roho yangu ikahangaika, ipate kuijua maana ya hiyo ndoto.

4Wakasidi wakamwambia mfalme kwa Kishami: E mfalme, na uwe mwenye uzima kale na kale! Waambie watumwa wako hiyo ndoto! ndipo, tutakapokueleza maana yake.[#Dan. 3:9.]

5Mfalme akawajibu, akawaambia Wakasidi: Neno langu lisilogeuzwa ni hili: msiponijulisha ndoto na maana yake, mtakatwa vipandevipande, nazo nyumba zenu zitabomolewa, ziwe vifusi.

6Lakini mkiweza kuieleza hiyo ndoto na maana yake, mtapata matunzo na vipaji na macheo makuu mbele yangu. Kwa hiyo ielezeni ndoto na maana yake!

7Wakajibu mara ya pili wakisema: Mfalme na awaambie watumwa wake ndoto! ndipo, tutakapoieleza maana.

8Mfalme akajibu kwamba: Mimi najua kweli, ya kuwa ninyi mnataka kujipatia siku, kwa kuwa mmeona, ya kama neno langu haligeuzwi.

9Kwani msipoijulisha hiyo ndoto, amri, nitakayoitoa kwa ajili yenu, ni ile moja; kwani mmepatana kuniambia maneno ya uwongo na ya madanganyo, mpaka siku nyingine zitokee. Kwa hiyo niambieni ile ndoto, nijue, ya kuwa mtanieleza nayo maana yake!

10Wakasidi wakamjibu mfalme kwamba: Hakuna mtu ulimwenguni anayeweza kulieleza hilo neno la mfalme; kwani hakuna mfalme ye yote, ingawa ni mkuu mwenye nguvu, aliyetaka jambo kama hilo kwao wote walio waandishi na waaguaji na Wakasidi.

11Jambo hili, mfalme analolitaka, ni zito, tena hakuna mtu awezaye kulieleza mbele yake mfalme, ni miungu tu, lakini haikai kwetu sisi tulio wenye miili ya kimtu.

12Ndipo, mfalme alipopatwa na machafuko makali sana, akaagiza, wajuzi wote wa Babeli wauawe.

13Amri hiyo ya kuwaua wajuzi ilipokwisha kutoka, wakamtafuta naye Danieli na wenziwe, wauawe.

14Ndipo, Danieli alipotumia akili zake zenye werevu, akasema na Arioki aliyekuwa mkuu wa walinzi wa mfalme, naye alikuwa ametoka kwenda kuwaua wajuzi wa Babeli.[#Dan. 1:17,20; 2:24.]

15Basi, akamwuliza Arioki, kwa kuwa ni mtu wa nguvu wa mfalme: Mbona amri hiyo kali imetoka kwake mfalme? Arioki alipomjulisha Danieli jambo hilo,

16Danieli akaingia kwa mfalme, akamwomba, ampe siku kidogo, apate kumweleza mfalme maana ya ndoto.

17Kisha Danieli akaingia nyumbani mwake, akawajulisha wenziwe Hanania na Misaeli na Azaria hilo jambo,

18wamwombe Mungu wa mbinguni, awahurumie kwa ajili ya hilo jambo lililofichika, Danieli na wenziwe wasiuawe pamoja na wajuzi wa Babeli.

19Kisha Danieli akafumbuliwa katika ono la usiku hilo jambo lililofichika; ndipo, Danieli alipomtukuza Mungu wa mbinguni.[#Dan. 2:30.]

20Hivi ndivyo, Danieli alivyosema: Jina lake Mungu litukuzwe kale na kale! Kwani yeye ni mwenye ujuzi na uwezo!

21Yeye ndiye anayezigeuza siku na miaka, ndiye anayeondoa wafalme, tena ndiye anayeweka wafalme, ndiye anayewapa wajuzi ujuzi, nao watambuzi huwapa utambuzi.[#Dan. 4:17,25,32.]

22Yeye ndiye anayefunua yasiyochunguzika nayo yaliyofichwa. Anayajua yaliyomo gizani, nao mwanga unakaa kwake.

23Wewe Mungu wa baba zangu, mimi ninakushukuru na kukusifu, kwa kuwa umenipa ujuzi na uwezo, ukanijulisha tuliyokuomba, ukanijulisha lile jambo la mfalme.

24Ndipo, Danieli alipokwenda kwake Arioki, mfalme aliyemwagiza kuwaua wajuzi wa Babeli; alipofika akamwambia: Wajuzi wa Babeli usiwaue! Ila nipeleke kwake mfalme, nimweleze mfalme maana ya ndoto![#Dan. 2:14.]

25Kisha Arioki akampeleka Danieli upesi kwake mfalme, akamwambia hivyo: Nimeona mtu, ni mmoja wao Wayuda waliotekwa na kuhamishwa kuja huku, ndiye atakayemjulisha mfalme maana ya ndoto.

26Mfalme akamwuliza Danieli aliyeitwa Beltesasari, akasema: Unaweza kunijulisha ndoto, niliyoiota, na kuniambia maana yake?

27Danieli akajibu masikioni pa mfalme, akasema: Fumbo, mfalme analolitaka, hakuna wajuzi wala waaguaji wala waandishi wala wachunguza nyota wanaoweza kumweleza mfalme maana yake.

28Lakini juu mbinguni yuko Mungu anayefunua mafumbo: yeye anamjulisha mfalme Nebukadinesari yatakayokuwa siku za mwisho. Ndoto yako na maono yaliyokuwa mbele yako, ulipolala kitandani, ndiyo haya:

29Wewe mfalme ulipolala kitandani, yakakuinukia mawazo ya mambo yatakayokuwa halafu; ndipo, yeye afunuaye mafumbo alipokujulisha yatakayokuwa.[#Dan. 2:22.]

30Mimi nami sikufunuliwa fumbo hilo kwa kwamba ninao ujuzi kuliko wengine walipo, ila ni kwa kwamba mfalme ajulishwe maana ya ndoto, upate kuyajua, uliyoyawaza moyoni.[#1 Mose 41:16.]

31Wewe mfalme ulikuwa ukiota, mara ukaona kinyago kimoja. Kinyago hicho kilikuwa kikubwa sana, kikametuka kabisa, kikasimama mbele yako, kikatia woga kwa kutazamwa tu.

32Hicho kinyago kichwa chake kilikuwa cha dhahabu tupu, kifua chake na mikono yake ilikuwa ya fedha, tumbo lake na viuno vyake vilikuwa vya shaba,

33mapaja yake yalikuwa ya chuma, miguu yake ilikuwa nusu ya chuma, nusu ya udongo.

34Ulipokuwa unakitazama, mara jiwe likaporomoka lenyewe lisilotupwa na mikono ya watu, likakipiga kile kinyago penye miguu yake iliyokuwa ya chuma na ya udongo, likaiponda.

35Ndipo, yote pia yalipopondeka kwa mara moja, chuma, udongo, shaba, fedha, dhahabu, yakawa kama makapi penye kupuria ngano siku za kiangazi, upepo ukayapeperusha, yakatoweka kabisa, hata mahali pao hapakujulika. Lakini lile jiwe lililokiponda kile kinyago likawa mlima mkubwa, ukaieneza nchi yote.

36Hii ndiyo ndoto, sasa tumwambie mfalme nayo maana yake:

37Wewe mfalme ndiwe mfalme wa wafalme, Mungu wa mbinguni amekupa ufalme na uwezo na nguvu na macheo makuu.[#Ez. 26:7.]

38Pote panapokaa watu na nyama wa porini na ndege wa angani amepatia mkononi mwako, uwatawale hao wote. Wewe ndiwe kichwa cha dhahabu.[#Yer. 27:6.]

39Nyuma yako utatokea ufalme mwingine usio na nguvu kama wako. Kisha utafuata ufalme wa tatu, ni wa shaba utazitawala nchi zote.

40Kisha utakuwa ufalme wa nne wenye nguvu kama za chuma; kama chuma kinavyovunja na kuponda vyote kabisa, ndivyo, utakavyoponda na kuuvunja ufalme wote mwingine kama chuma chenye kuvunja.

41Lakini hivyo, ulivyoiona miguu yake na vidole vyake kuwa nusu yao ya udongo na nusu yao ya chuma, utakuwa ufalme uliogawanyika: upande utakuwa wenye nguvu za chuma, sawasawa kama ulivyoona chuma kilichochanganyika na udongo wa mfinyanzi.

42Navyo vidole vya miguu yake nusu yao ni ya chuma nusu yao nyingine ni ya udongo, ni kwamba: Upande wa ufalme huo utakuwa wenye nguvu, lakini upande utakuwa unavunjikavunjika.

43Tena umeona, chuma kilivyochanganyika na udongo wa mfinyanzi, ni kwamba: Wao watajichanganyachanganya na vizazi vya watu kwa kuoana, lakini hawataambatana mtu na mwenziwe, kama chuma kisivyochanganyikana na udongo.

44Siku zile za wafalme hao Mungu wa mbinguni atatokeza ufalme usioangamika kale na kale, usiochukuliwa tena na kabila jingine, nao utauponda ufalme wote mwingine na kuutowesha, lakini wenyewe utakaa kale na kale,[#Dan. 7:14,27; Yes. 9:7; 1 Kor. 15:24; Ufu. 11:15.]

45kama ulivyoliona lile jiwe, likiporomoka toka mlimani lenyewe lisilotupwa na mikono ya watu, likaponda chuma na shamba na udongo na fedha na dhahabu. Mungu aliye mkuu amemjulisha mfalme yatakayokuwa siku zitakazokuja. Ndoto hii ni ya kweli kabisa, nayo maana yake inategemeka.[#Dan. 2:34.]

46Ndipo, mfalme Nebukadinesari alipoanguka kifudifudi, kisha akamwinamia Danieli, akaagiza kumtolea vipaji vya tambiko na uvumba.

47Kisha mfalme akamwambia Danieli akisema: Kweli Mungu wenu ni Mungu aipitaye miungu yote, ni Bwana wa wafalme, maana huyafunua yaliyofichwa, kwa hiyo umeweza kulifunua hili fumbo.[#Dan. 3:29; Yos. 2:11; Sh. 86:8; Yes. 42:8-9.]

48Kisha mfalme akampa Danieli macheo na matunzo mazuri mno, mengi sana, akampa nalo jimbo lote la Babeli, alitawale, awe mkuu wao watawala nchi wa kuwaamrisha wajuzi wote wa Babeli.[#Dan. 2:6.]

49Danieli alipomwomba mfalme, akawaagizia akina Sadiraki na Mesaki na Abedi-Nego kazi ya kuliangalia jimbo la Babeli, naye Danieli akakaa jumbani mwa mfalme.[#Dan. 3:12.]

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania