The chat will start when you send the first message.
1Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako,
Kabla hazijaja siku zilizo mbaya,
Wala haijakaribia miaka utakaposema,
Mimi sina furaha katika hiyo.
2Kabla jua, na nuru, na mwezi,
Na nyota, havijatiwa giza;
Kabla ya kurudi mawingu baada ya mvua;
3Siku ile walinzi wa nyumba watakapotetemeka;[#Zab 71:9; Zek 8:4; 2 Kor 5:1; Mwa 27:1]
Hapo wenye nguvu watakapojiinamisha;
Na wasagao kukoma kwa kuwa ni haba;
Na hao wachunguliao madirishani kutiwa giza;
4Na milango kufungwa katika njia kuu;[#Mik 7:1; 2 Sam 19:35]
Sauti ya kinu itakapokuwa ni ndogo;
Na mtu kushtuka kwa sauti ya ndege;
Nao binti za kuimba watapunguzwa;
5Naam, wataogopa kilichoinuka[#Law 19:32]
Na vitisho vitakuwapo njiani;
Na mlozi utachanua maua;
Na panzi atakuwa ni mzigo mzito;
Na pilipili hoho itapasuka;
Maana mtu aiendea nyumba yake ya milele,
Nao waombolezao wazunguka njiani.
6Kabla haijakatika kamba ya fedha;
Au kuvunjwa bakuli la dhahabu;
Au mtungi kuvunjika kisimani;
Au gurudumu kuvunjika birikani;
7Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa,[#Mwa 3:19; Mhu 3:21; Mwa 2:7; Hes 16:22]
Nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa.
8Mhubiri asema, Ubatili mtupu; mambo yote ni ubatili!
9Lakini, kwa sababu huyo Mhubiri alikuwa na hekima, aliendelea kuwafundisha watu maarifa, naam, akatafakari, akachunguza, akatunga mithali nyingi.
10Huyo Mhubiri akachunguza ili apate kuona maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.
11Maneno yao wenye hekima huwa mfano wa michokoo; na kama misumari iliyogongomewa sana; ndivyo yalivyo maneno yao walio wakuu wa makusanyiko, ambayo yatoka kwa mchungaji mmoja.
12Tena, zaidi ya hayo, mwanangu, kubali maonyo; hakuna mwisho wowote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.
13Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa;
Mche Mungu, nawe uzishike amri zake,
Maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.
14Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.[#Mt 12:36]