Zekaria 11

Zekaria 11

1Ifungue milango yako, Ee Lebanoni,

Ili moto uiteketeze mierezi yako.

2Piga yowe, msonobari, maana mwerezi umeanguka,

Kwa sababu miti iliyo mizuri imeharibika;

Pigeni yowe, enyi mialoni ya Bashani,

Kwa maana msitu wenye nguvu umeangamia.

3Sikiza, maombolezo ya wachungaji,

Kwa maana utukufu wao umeharibiwa;

Sikiza, ngurumo za simba,

Kwa maana vichaka vya Yordani vimeharibiwa!

Aina mbili za wachungaji

4BWANA, Mungu wangu, alisema hivi, Lilishe kundi la machinjo,

5ambalo wenye kundi hilo huwachinja, kisha hujiona kuwa hawana hatia; na hao wawauzao husema, Na ahimidiwe BWANA, kwa maana mimi ni tajiri; na wachungaji wao wenyewe hawawahurumii.[#Kum 29:19; Yer 2:3; Hos 12:8; Yn 16:2; 1 Tim 6:9; 2 Pet 2:3]

6Maana mimi sitawahurumia tena wenyeji wa nchi hii, asema BWANA; bali, tazama, nitawatia, kila mmoja wao, mikononi mwa mwenzake, na mikononi mwa mfalme; nao wataipiga hiyo nchi, wala mimi sitamwokoa yeyote kutoka kwa mkono wao.

7Basi nikalilisha kundi la machinjo, kweli kondoo waliokuwa wanyonge kabisa.[#Sef 3:12; Mt 11:5]

Kisha nikajipatia fimbo mbili; nami nikaiita ya kwanza, Neema, na ya pili nikaiita, Umoja; nikalilisha kundi lile.

8Nami nikawakatilia mbali wachungaji watatu katika mwezi mmoja; maana nafsi yangu ilikuwa imechoka kwa ajili yao, na nafsi zao pia walinichukia.[#Hos 5:7]

9Ndipo nikasema, Sitawalisheni; afaye na afe; atakayekatiliwa mbali na akatiliwe mbali; nao waliosalia, kila mmoja na ale nyama ya mwili wa mwenziwe.[#Yer 15:2]

10Nikaitwaa hiyo fimbo yangu, iitwayo Neema, nikaikata vipande viwili, ili nipate kulivunja agano langu nililolifanya na watu wa kabila zote.

11Nayo ikavunjwa siku ile; na hivyo wale kondoo wanyonge walionisikiliza wakajua ya kuwa neno hili ndilo neno la BWANA.

12Nikawaambia, Mkiona vema, nipeni ujira wangu; kama sivyo, msinipe. Basi wakanipimia vipande thelathini vya fedha, kuwa ndio ujira wangu.[#Kut 21:32; Mt 26:15]

13Kisha BWANA akaniambia, Mtupie mfinyanzi kima kizuri, hicho nilichotiwa kima na watu hao. Basi nikavitwaa vile vipande thelathini vya fedha, nikamtupia huyo mfinyanzi ndani ya nyumba ya BWANA.[#Mt 27:9-10]

14Ndipo nikaikata vipande viwili fimbo yangu ya pili, iitwayo Umoja, ili nipate kuuvunja udugu uliokuwa kati ya Yuda na Israeli.

15BWANA akaniambia, Jitwalie tena vyombo vya mchungaji mpumbavu.[#Eze 34:2]

16Kwa maana, tazama, mimi nitainua katika nchi hii mchungaji, ambaye hatawaangalia waliopotea, wala hatawatafuta waliotawanyika, wala hatamganga aliyevunjika, wala hatamlisha aliye mzima; bali atakula nyama ya wanono, na kuziraruararua kwato zao.

17Ole wake mchungaji asiyefaa, aliachaye kundi! Upanga utakuwa juu ya mkono wake, na juu ya jicho lake la kulia; mkono wake utakuwa umekauka kabisa, na jicho lake la kulia litakuwa limepofuka.[#Yer 23:1; Yn 10:12; Mik 3:6]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya